Mkutano wa mwaka wa Bunge la Umma la China na ule wa Baraza la Mashauriano ya Kisiasa la China ambayo inatarajiwa kufunguliwa kwa nyakati tofauti jumamosi wiki hii na jumatatu wiki ijayo, imetoa nafasi kwa wanahabari kukusanya na kutoa habari na uchambuzi wa mwelekeo wa China.
Beli ni mkurugenzi wa tawi la televisheni ya ETV ya Afrika Kusini hapa Beijing, hii ni mara yake ya nne kukusanya habari kuhusu mikutano hiyo miwili ya mwaka. Amesema anavutiwa na habari za China kwa sababu nchi nyingi zinazoendelea zinakabiliwa na changamoto sawa na China. Ameongeza kuwa, televisheni yake inafuatilia mageuzi ya mfumo wa matibabu na mambo ya elimu nchini China, kwa mfano jinsi gani China inavyowasaidia wahitimu wa vyuo vikuu kutafuta ajira.
Pamoja na kuwepo kwa hali yenye utatanishi duniani, mwanahabari huyo kutoka Afrika Kusini amesema ana imani na uchumi wa China ambao maendeleo yake yatainufaisha dunia nzima. Amesema Afrika Kusini ni nchi yenye utajiri mkubwa wa maliasili, na ongezeko la uchumi wa China litaisaidia Afrika Kusini kusafirisha zaidi maliasili yake nje ya nchi.
Katika mikutano miwili ya mwaka huu, Bw Beli amesema anapenda kuuliza maswali kama vile kujua kama China ina mpango wa kuongeza uwekezaji barani Afrika katika sekta za madini, ujenzi wa miundo mbinu, sayansi na teknolojia pamoja na mambo ya fedha.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |