• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • barua 0528

    (GMT+08:00) 2013-06-03 15:48:27
    Barua ya kwanza inatoka kwa msikilizaji wetu Gulam Haji Karim wa S.L.P 504 Lindi Tanzania anaanza kwa kusema siku ya Jumatatu ni siku ya pili ya ziara ya rais Xi Jinping wa China nchini Tanzania. baada ya kusalimiana walianza shughuli za ziara hiyo kwa ufunguzi wa ukumbi wa kimataifa wa Julius Nyerere ambao ni wa kisasa kabisa uliogharamiwa na serikali ya China. Katika ufunguzi huo rais Xi alimwaga sera zake kwa Afrika na kuahidi kutoa misaada kwa nchi mbalimbali za Afrika na tayari China imetenga dola bilioni 20 kwa mwaka 2013/2014.

    Baada ya kutangaza sera alimalizia kwa kumkabidhi funguo za jengo hilo lenye ghorofa tatu rais Jakaya kikwete na mwishowe kuzuru makaburi ya wataalamu wa China waliofariki Tanzania na kuweka mashada ya maua, ambapo jioni ya siku hiyo aliondoka kwa ndege ya Boeng 747 na kuelekea Afrika Kusini. Namtakia kila la heri kiongozi huyu, ahsante sana.

    Tunakushukuru kwa dhati msikilizaji wetu Gulam Haji Karim kwa barua yako kuhusu ujio wa rais Xi Jinping nchini Tanzania. kwa kweli hatua ya rais huyu, kuifanya Tanzania kuwa kituo chake cha kwanza katika nchi za Afrika inaonesha kuwa China inaithamini sana Tanzania na ni marafiki wakubwa sana, sisi kwa upande wetu tunauombea ushirikiano huu uendelee kudumu, ahsante sana.

    Barua nyingine inatoka kwa msikilizaji wetu Bi Halima Ijeiza wa S.L.P 14-40602 Ndori Kenya anasema pokeeni salamu zangu za dhati nikitumai hali yenu ni shwari, mimi huku sina neno mbali na kulilia mvua kwani jua sasa limewaka na kusababisha kiangazi kwa zaidi ya miezi mitatu. Nataka kutoa shukrani zangu kwenu kwa kunitumia kadi za salamu ambazo ndizo zimejaa kuliko zile zenye picha, bahasha iliyolipwa pamoja na kalenda ya mwaka huu wa 2013, nashukuru pia kwa mawasiliano ya mara kwa mara baina yetu.

    Baada ya hapo ningependa kujua kwanini hamjaanzisha tena shindano la chemsha bongo mwaka huu? Chombo hiki hutuunganisha sisi mashabiki kote ulimwenguni, mbali na kutupa nafasi ya kujishindia zawadi mbalimbali na hata nafasi maalumu. Hata hivyo ninaendelea kufurahia vipindi vyenu mbalimbali. Ahsante sana.

    Shukran za dhati msikilizaji wetu Bi Halima Ijeiza kwa barua yako, nasi tunashukuru kwa kuunga mkono, ila kuhusu chemsha bongo kwa sasa bado hatujatoa mpya, ila usiwe na wasiwasi tutakapotoa shindano jipya kila msikilizaji wetu atapata taarifa, ahsante sana.

    Sasa ni zamu ya msikilizaji wetu Mutanda Ayubu Sharif wa S.L.P 172 Bungoma Kenya anasema salamu kwa wafanyakazi wote wa CRI, bila kusahau wasikilizaji wote popote walipo, nawasihi mnipe masikio na macho yenu kwa dakika chache. Ningependa kuandika shairi hili kwani imekuwa jambo la kukera sana kwa visa vya wanawake kuwachapa waume zao vinaendelea hapa mjini hasa mkoa wa kati. Ninaamini kuwa sio vyema watu wapendanao kupigana kwa kiwango cha kuwaacha wenzao na majeraha mabaya ya moto, panga au kisu, hii yote ni dhambi, maovu na makosa makubwa. Waume mmewakosea nini wake zenu, na wewe mke ni vyema kweli hivyo mnavyofanya.

    Kwa jina lake jalia, muumba aso na ila

    Kwa ulingo najitia, kukemea waso mila

    Pengine watasitia, kukemea fadhila

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Najua mke ni nguzo, kwa myumba ili kufaa

    Husimama kwa mkazo, msingi wake ni bwana

    Pindi huwa ni tatizo, msingi napoachana

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Haya nisingemaizi, ni mambo Kenya ya kati

    Ni mke au jambazi, ama mnatuzwa vyeti

    Mnaikata mizizi, na uzazi una kiti

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Mmekiuka unyago, dini na utamaduni

    Raha mwaipa magongo, kiwa bado duniani

    Hata awe ni utingo, mke ni mme nyumbani

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Sitawalaumu sana, pengine mwakosa funzo

    Japo mngesoma sana, ndoa ina lake tunzo

    Kuoana si hiyana, si kufanya mabonzo

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Sasa nina wausia, enyi mtokeao kati

    Ya mume kikuzidia, mchape na lako titi

    Mwishowe atasinzia, mbinu ya kumdhibiti

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Na nyumba iso msingi, hatimaye huanguka

    Yatakutatiza mengi, mwishowe kufadhaika

    Haikufai kwa wingi, ila unapumbazika

    Mke achapaye bwana, ni nyumba iso msingi

    Tunakushuru sana msikilizaji wetu Mutanda Ayubu Sharif kwa shairi lako zuri lenye mafunzo kemkem, ni kweli si tabia njema kwa wanawake kuwapiga waume zao, kwani huo si uungwana hata kidogo, raha ya ndoa ni masikilizano na kama masikilizano hayapo ni vyema kuwashirikisha wazee ili watatue kasoro zilizopo na sio kutwangana mangumi ahsante.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako