Mshambuliaji wa Uruguay Luis Suarez amefungiwa kushiriki shughuli zozote zinazohusiana na soka kwa miezi mine, kufuatia kashfa ya kumng'ata mlinzi wa Italy Giorgio Chiellini. Zaidi ya hayo mchezaji huyo wa Liverpool mwenye miaka 27 amefungiwa kucheza mechi 9 za kimataifa, hivyo hatacheza mechi zilizosalia za kombe la dunia na pia atakosa mechi 9 za mwanzo za msimu mpya wa ligi ya Uingereza. Kufuatia adhabu hiyo iliyotolewa na kamati ya nidhamu ya Fifa, rais wa chama cha soka cha Uruguay Wilmar Valdez amesema watakata rufaa kwa kile wanachodai kuwa hakuna ushahidi wa kutosha na pia adhabu iliyotolewa ni kali mno. Suarez pia ametozwa faini ya pauni 65,680 kwa kitendo chake hicho. Adhabu hiyo ya Suarez ni kubwa katika historia ya michuano ya kombe la dunia na kuishinda ile aliyopewa mchezaji wa Italia Mauro Tassotti kwa kumpiga kiwiko kwa nguvu mchezaji mwenzake mwaka 1994.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |