Timu ya mbio za magari ya langa langa ya Marussia ya Formula One "wameshtushwa na kukasirishwa" na ripoti kutoka baadhi ya vyombo vya habari inayosema kuwa Jules Bianchi hakupunguza mwendo kwenye vibendera vya tahadhari wakati wa mashindano ya Japanese Grand Prix. Bianchi, mwenye umri wa miaka 25, amelazwa hospitali kutokana na kujeruhiwa vibaya kichwani baada ya kupata ajali akiwa kwenye mashindano hayo. Marussia pia wamekana madai kwamba walimwambia Bianchi kuendesha kwa kasi wakati wa kipindi cha tahadhari ili kumweka nyuma mpinzani wake. Marussia imeamua kutoa taarifa yake baada ya kile walichokielezea kuwa "ripoti za vyombo vya habari zinazotofautiana" zimezusha kuhoji uamuzi wa Bianchi na timu ya Marussia katika uwanja wa Suzuka. Jules hakupunguza mwendo katika eneo la bendera za njano zilipoonyeshwa mara mbili, imesema taarifa hiyo. "Huo ni ukweli usiopingika, kama takwimu zinavyoeleza, ambazo timu hii imetoa kwa Shirikisho la FIA. Charlie Whiting, mkurugenzi wa mbio za FIA, amethibitisha kuwa timu ya Marussia ilitoa takwimu kama hizo, kwamba alipitia takwimu hizo na kwamba Jules alipunguza mwendo. Jumatatu familia ya Bianchi ilisema dereva huyo mwenye umri wa miaka 25 alikabiliwa na "changamoto kadha" za matibabu tangu ajali hiyo na hali yake inazidi kuwa mbaya. Mapema siku hiyo baba yake, Bianchi, Philippe alielezea hali ya mtoto wake kuwa ya "kukatisha tamaa" lakini alisema alijua mtoto wake "hatakata tamaa" katika kupigania uhai wake.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |