Umoja wa Mataifa umeitaka Korea Kaskazini ichukue hatua zote kupunguza hali ya wasiwasi kwenye peninsula ya Korea na kurudi kwenye mazungumzo ya amani na kuondoa silaha za nyuklia. Msemaji wa umoja huo Bw. Stephane Dujarric amesema Umoja wa Mataifa ina wasiwasi mkubwa kutokana na mvutano unaoongezeka kwenye Peninsula ya Korea, na kutoa wito kwa pande zote kuongeza juhudi za kidiplomasia na kuhakikisha maazimio ya umoja huo yanatekelezwa kikamilifu.
Jana naibu balozi wa Korea Kaskazini katika Umoja wa Mataifa alisema kuwa nchi hiyo inalaani na kususia mkutano wa Baraza la usalama kuhusu suala la nyuklia la Korea Kaskazini utakaofanyika tarehe 28 mwezi huu, akiutaja mkutano huo kuwa ni uvamizi dhidi ya mamlaka ya nchi yake unaodhibitiwa na Marekani.
Kuhusu suala hilo, Marekani imesema haitafuti mgogoro na Korea Kaskazini na nia yake ni kuitaka nchi hiyo iache mpango wake wa kuendeleza silaha za nyuklia, na kwa upande wake Russia inaitaka Marekani isichukue hatua ya upande mmoja dhidi ya nchi hiyo kama ilivyofanya nchini Syria.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |