Kenya imenyang'anywa fursa ya kuandaa mashindano ya ubingwa wa Afrika wa mwaka 2018 (CHAN) kufuatia mkutano wa kamati kuu ya shirikisho la mpira wa miguu barani Afrika (CAF) uliofanyika Accra Ghana ukiongozwa na rais wa shirikisho hilo, Ahmad Ahmad.
CAF imesema uamuzi huo umechukuliwa baada ya kuchelewa kwa ripoti za ukaguzi kadha uliofanywa nchini Kenya.
Timu ya ukaguzi ya CAF ilizuru Kenya kuanzia tarehe 11 hadi 17 mwezi huu, na kukuta kiwanja kimoja kati ya viwanja vinne ndio kipo tayari kwa michuano hiyo.
Shirikisho la kandanda nchini Kenya (FKF) linasisitiza kuwa lilifanya kila liwezalo kuhakikisha kuwa mashindano ya CHAN mwaka 2018 yangewezekana kwa Kenya na eneo lote la Afrika Mashariki.
Kinyanganyiro hicho ambacho kitashirikisha timu 16 kinatarajiwa kuanza tarehe 12 Januari hadi Februari mwaka 2018.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |