Waziri Mkuu wa Libya anayeungwa mkono na Umoja wa mataifa Bw. Fayez Serraj amesema anaunga mkono mpango wa utekelezaji kuhusu mpito wa kisiasa uliopendekezwa na tume ya umoja wa mataifa nchini Libya.
Bw Serraj amesema hayo baada ya kukutana na mkuu wa tume hiyo Bw Ghassan Salame, na kufanya naye mazungumzo kuhusu maendeleo ya kisiasa nchini Libya. Amesema anaunga mkono hatua zilizochukuliwa hadi sasa kutekeleza kipindi cha mpito, kitakachofuatiwa na kufanyika kwa uchaguzi wa rais na wabunge kabla ya mwisho wa mwaka huu, na kuanza kuijenga upya Libya yenye utulivu.
Hatua ya kwanza ya utekelezaji wa mpito wa kisiasa nchini Libya inahusisha makubaliano ya kati ya miji ya Misurata na Tawergha. Wakazi wa Tawergha waliowaunga mkono wapiganaji wa aliyekuwa kiongozi wa Libya Muamar Gaddafi, walilazimika kukimbia mji wao baada ya kushindwa kwenye mapambano.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |