• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Wawekezaji wa China wasaidia kuongeza kawi safi Kenya

    (GMT+08:00) 2018-02-21 17:45:00

    Uwekezaji wa kawi endelevu nchini Kenya kutoka China unatarajiwa kuendelea kusaidia nchi hiyo ya Afrika Mahariki kukabili changamoto za mahitaji yanayoongezeka ya umeme na pia kupunguza gharama.

    Hadi sasa makampuni ya China yamewekeza kwenye miradi kadhaa ya kawi safi ikiwemo kawi ya jua kaunti ya Garisa, kawi ya upepo katika eneo la kipeto kaunti ya Kajiado na kawi ya mvuke katika eneo la Ol Karia kaunti ya Nakuru.

    Kwenye mfululizo wetu wa makala za uwekezaji wa kawi safi nchini humo tunakuletea kwanza ripoti yake Ronald Mutie kuhusu uwekezaji wa kawi ya mvuke wa dola milioni 94.

    Vijana wanafanya kazi ya kuchomelea vyuma katia eneo la viwanda vidogo nje ya mji wa Naivasha, killomita 120 hivi kutoka mji mkuu Nairobi.

    Kuwepo na umeme wa kutosha kumehakikisha vijana hawa wanaendelea na kazi yao mchana kutwa na hivyo kuinua hali yao ya maisha.

    Serikali ya Kenya kuanzia mwaka 2013 ilianzisha kampeni ya "Last Mile" ikilenga kufikisha umeme katika maneo yote nchini humo.

    Lakini huku serikali ikiwa mbioni kusambaza umeme, kiwango ambacho kinazalishwa ni chini ya megawati 3,000.

    Hivyo baadhi ya wakati wafanyabiashara kama vijana hawa wanalamika kuhusu gharama ya juu ya huduma za umeme.

    "Nalipa pesa nyingi kwa ajili ya kawi naona inaniumiza sana"anasema mmoja wa wakaazi.

    Ili kuongezea umeme unaozalishwa na hatimaye kupunguza bei kwa wateja, serikali ilianza kuwekeza kwenye miradi mikubwa.

    Lakini miradi inayotegemea mito pia ilikabiliwa na changamoto wakati wa kiangazi huku ile ya dizeli ikiwa inachafua mazingira.

    Hivyo serikali iliaamua kuwekeza zaidi kwenye vyanzo endelevu kama vile jua, upepo na mvuke.

    Bwana Albert Mugo meneja mkurungezi wa shirika la kuzalisha kawi nchini Kenya Kengen anafahamu kukiwa na vyanzo vingi vya umeme huduma inaweza kufikia kila mtu kwa bei nafuu.

    "Kuna nafasi zaidi ya kuwa na kawi endelevu. Tuna miradi ya kawi ya jua na upepo, lakini sio mikubwa kama vile kawi ya mvuke. Uzuri wa kawi ya mvuke ni kwamba ni ya kutegemewa, inapatikana wakati wote, lakini jua ama upepo ni tofauti kwa sababu kuna wakati hakuna jua kama usiku, au hakuna upepo. Lakini hata hivyo, kwenye mfumo mzuri wa kawi, ni vyema kuwa na usawa ili chanzo kimoja kikikoskana unaweza kutumia kingine "

    Kenya ina uwezo wa kuzalisha angalau megawati 10,000 za kawi ya mvuke kwenye eneo la bonge la ufa.

    Hata hivyo hadi sasa Kenya imezalisha megawati 600 tu kutokana na mvuke.

    Kuwekeza kwenye miradi ya mvuke kunahitaji, mitaji mikubwa na hivyo serikali inategemea wawekezaji wa kibinafsi kama kampuni hii ya Yantai Jereh kutoka China ambayo tayari imetia saini na serikali ya Kenya kuzalisha megawati 53 za kawi ya mvuke katika eneo la Ol karia.

    Ufadhili wa dola milioni 94.5 wa mradi huo umetolewa na benki ya viwanda na biashara ya China.

    Charles Keter ni waziri wa kawi nchini Kenya.

    "Ningependa kuishukuru serikali ya China kwa kusaidia juhudi zetu za kuwa na kawi endelevu. Kwa mara ya kwanza tutakuwa na ajira kijani, yaani zaidi ya watu 3000 wataajiriwa kwenye mradi huu. Pia sasa tutakuwa na kawi safi isiochafua mazingira, hivyo naona huu ni mradi wenye athari chanya"

    Na kuhusu swala la mtaji waziri Keter anasema.

    "Hatuna pesa za kuwekeza lakini tuna mvuke, nao wachina wana pesa za kutekeleza mradi huu, hivyo tunatahmini jinsi ya kushiriki pamoja mradi huu kwa kuwaruhusu kumiliki kiasi Fulani cha hisa. Kwa njia hiyo hatutatumia fedha kutoka kwa serikali. Mahitaji ya kawi bado ni mengi kwa sababu kuna baadhi ya miradi inayozalisha kawi kwa kutumia dizeli ambayo ni ghali sana"

    Wakati wa kuapishwa kwa muhula wa pili rais wa Kenya Uhuru Kenyatta aliahidi kuwa atapunguza kwa nusu ada ya kawi inayotozwa watengenezaji bidhaa.

    Hata hivyo anasema ili kuwa na kawi ya kutosha serikali itahitaji kuwekeza zaidi hasa kwenye kawi ya mvuke.

    "Kuzalisha kawi endelevu kama vile kawi ya mvuke ni hatua ya kwanza ya kutatua changamoto za mabadiliko ya tabia nchi . Hakuna chanzo cha kawi kijani kilicho bora kuliko kawi ya mvuke. Tayari sisi ni miongoni mwa wazlishaji 10 wakuu wa kawi ya mvuke kote duniani na raslimali yetu ya kawi hiyo ni miongoni mwa kubwa duniani"

    Kufikia mwaka 2015 kenya ilikuwa na jumla ya megawati 2,299 za kawi.

    Kati ya kiwango hicho asilimia 60 ni kawi ya mvuke, asilimia 39 kawi ya maji ma asilimia 1 upepo.

    Lakini mpango wa serikali ni kuendelea kupunguza utegemezi wa vyanzo ghali na vinavyochafua mazigira na badale yake kuongeza uwekezaji kwenye miradi kama huu wa kampuni ya China ya Yantai Jereh.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako