Chama cha wahudumu wa magari ya usafiri wa umma maarufu matatu jijini Nairobi kimepinga vikali kuanzishwa kwa huduma za uchukuzi wa mabasi ya Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) kikidai hatua hiyo inalenga kuhujumu oparesheni zao.
Mwenyekiti wa Chama hicho Jimal Ibrahim alikosoa hatua hiyo akisema kuwa si haki kwa serikali kuanzisha huduma hiyo.
Alisema serikali ingetoa fedha zaidi ili kurekebisha barabara katika mitaa kama vile Juja,Mwiki,Komarock na mitaa mingine jijini.
Mabasi takriban 27 yameanza kuhudumu katika baadhi ya mitaa jijini Nairobi,ambapo serikali inasema inalenga kulainisha sekta ya uchukuzi.
Kulingana na Mkurugenzi wa Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) Richard Ndubai,mabasi hayo yatahudumu katika maeneo ya Kibera,Githurai,Mwiki,Mukuru kwa Njenga,Dandora,Kariobangi na Kawangware.
Mabasi hayo yatakuwa yakiwatoza abiria nauli ya Sh50 kila wakati ili kuwazuia dhidi ya kupunjwa na wahudumu wa matatu ambao hupandisha nauli mara kwa mara.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |