Vikosi vya Umoja wa Afrika vya kulinda amani nchini Somalia vimetangaza kuanza kwa zoezi la kuwasajili kwa njia ya kielektroniki wanajeshi wa vikundi vya kikabila katika eneo la Jubbaland, ikiwa ni mwendelezo wa kuunganisha vikosi vya usalama katika eneo hilo.
Akizungumza mjini Kismayo, Mratibu wa vikosi vya AMISOM Martin Abili amesema zaidi ya wanajeshi 5000 wa vikundi hivyo watasajiliwa katika miji ya Gedo, Juba Kusini na Jubba ya Kati.
Amesema usajili huo wa kielektroniki unalenga kukusanya taarifa binafsi za msingi ikiwemo picha, na alama za vidole za kila mwanajeshi.
Abili amefafanua kwamba wanajeshi hao wataambatanishwa na polisi wa mjini Jubbaland, au majeshi ya ziada ama Jeshi la serikali la Somalia.
Naye Kamanda wa Jeshi la Jubbaland Brigedia Jenerali Adam Mohamud Ibrahim amesema zoezi hilo ni muhimu katika eneo hilo. Na wako tayari kusaidia ili usajili huo ukamilike.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |