Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya amefanya mazungumzo na mwenzake wa Somalia Bw. Mohamed Abdullahi Farmajo mjini Nairobi kuhusu masuala ya usalama.
Ikulu ya Kenya imesema viongozi hao wamejadili uhusiano wa pande mbili na masuala ya usalama ikiwemo kuendelea kuiunga mkono Tume ya Umoja wa Afrika nchini Somalia AMISOM, ambayo vikosi vya Kenya vinachukua nafasi kubwa. Pia wamefahamishana kuhusu maendeleo mapya ya kila upande katika masuala ya usalama wanayofuatilia kwa pamoja na juhudi zinazofanywa na Kenya na nchi nyingine kurudisha amani na utulivu nchini Somalia.
Na polisi wa Kenya wametangaza kutoa zawadi ya dola za kimarekani elfu 30 kwa taarifa zozote zitakazosaidia kukamatwa kwa watuhumiwa watatu wa ugaidi kutoka Somalia wanaopanga kutekeleza mashambulizi katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.
Wakati huohuo, mamlaka za Kenya zimejenga kambi za ziada za usalama katika maeneo yanayodhaniwa kulengwa na kundi la al-Shabaab kufanya mashambulizi katika mji wa pwani wa Lamu, ili kuondoa uwezekano wa kutokea kwa mashambulizi mjini humo.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |