Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa na mkuu wa tume ya Umoja huo nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC MONUSCO Bibi Leila Zerrougui amesema maendeleo makubwa yamepatikana kwenye maandalizi ya uchaguzi utakaofanyika nchini DRC, lakini mazingira ya kuhakikisha ushindani wa haki bado hayajakuwa ya kuridhisha.
Bibi Zerrougui ameliambia baraza la usalama la Umoja huo kuwa, ingawa maendeleo makubwa yamepatikana kwenye kuheshimu mchakato wa kalenda, lakini mchakato wa uchaguzi bado unakabiliwa na hali ya kutoaminiana kati ya chama tawala na upinzani, vyama vya upinzani na tume huru ya uchaguzi CENI.
Ameeleza kuwa maandalizi hayo yamefikia hatua muhimu ya kufunguliwa kwa ofisi ya kupokea fomu za wagombea urais na wabunge, katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika Desemba 23 mwaka huu. Hata hivyo amesema wapinzani wametoa malalamiko mengi kuhusu mashine ya kuhesabia kura na uandikishaji wa wapiga kura.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |