• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Mpango wa China wa kupambana na malaria wawanufaisha watu wa Afrika

    (GMT+08:00) 2018-08-31 09:15:23

    Mwezi Desemba mwaka 2015, kwenye mkutano wa kilele wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika FOCAC uliofanyika Johannesburg, Afrika Kusini, rais Xi Jinping wa China alitangaza kuinua kiwango cha uhusiano kati ya China na Afrika kuwa uhusiano wa wenzi wa ushirikiano wa kimkakati wa pande zote, na kutoa mipango 10 mikubwa ya ushirikiano katika sekta za viwanda, kilimo, miundombinu, fedha, maendeleo yasiyoleta uchafuzi wa mazingira, kurahisisha biashara na uwekezaji, kuondoa umaskini na kuwanufaisha watu, afya, utamaduni, amani na usalama. Leo tutakuletea sehemu ya nane iitwayo "Mpango wa China wa kupambana na malaria unawanufaisha watu wa Afrika".

    Malaria ni ugonjwa unaoambukizwa na mbu wa jenasi Anopheles na kusababishwa na kidubini aina ya protisti Plasmodium, ambao unawaathiri vibaya watu. "Ripoti ya hali ya ugonjwa wa malaria duniani ya mwaka 2017" iliyotolewa na Shirika la Afya Duniani WHO imeonyesha kwamba katika mwaka 2016, idadi ya wagonjwa wapya duniani walioambukizwa malaria ilifikia milioni 216, ambayo imeongeza kwa takriban watu milioni 5 ikilinganishwa na idadi ya mwaka 2015. Katika mwaka 2016, idadi ya vifo vya wagonjwa wa malaria duniani kote imefikia laki 4.45, na idadi ya vifo na wanaoambukizwa malaria barani Afrika bado imechukua asilimia 90 ya idadi ya jumla ya duniani kote. Kutafuta ufumbuzi wa kukinga na kuondoa ugonjwa wa malaria mapema iwezekanavyo kumekuwa suala linalofuatiliwa sana kwenye sekta ya afya duniani kote.

    Tangu mwaka 2007, kundi la kukinga ugonjwa wa malaria kutoka Chuo Kikuu cha Matibabu ya Kichina cha Guangzhou lilitekeleza "Mpango wa China wa kupambana na malaria" nchini Comoro, ambao ni mpango unaolenga kuondoa chanzo cha maambukizo ya malaria kwa kutumia dawa ya Artemisinin inayotengenezwa na China. Kwa mujibu wa fikra ya undani wa matibabu ya Kichina, mpango huo unatumia dawa ya Artemisinin katika kukinga ugonjwa wa malaria, ambao watu wote wanatumia dawa na kuepusha ugonjwa huo kwa pamoja, na umepata mafanikio makubwa. Mkuu wa Idara ya Udaktari wa Kitropiki katika Chuo Kikuu cha Matibabu ya Kichina cha Guangzhou Profesa Song Jianping amesema "Mpango wa China wa kupambana na malaria" umeunganisha maarifa ya kichina na hali halisi ya mlipuko wa ugonjwa wa malaria barani Afrika, ambao unaweza kufanya kazi vizuri katika kudhibiti na kusimamisha mlipuko wa malaria ndani ya muda mfupi.

    "Kuna changamoto kadhaa zinazoikabili Afrika katika kukinga ugonjwa wa malaria. Ya kwanza ni kutokuwepo kwa dawa, yaani mfumo wa hivi sasa hauwezi kuwapatia wagonjwa wa malaria matibabu ya haraka; Ya pili, hali ya kimsingi ya hivi sasa kwenye sekta ya afya ya umma haiwezi kuboreshwa ndani ya muda mfupi; Ya tatu, ufumbuzi wa kudhibiti na kuondoa malaria kwa kupitia kuzuia na kuangamiza mbu hauwezi kufanya kazi kikamilifu. Tangu mwaka 2007, kundi letu tulifika Comoro na kutumia dawa ya kichina Artemisinin katika visiwa vitatu nchini humo kwa kupitia vipindi vitatu. Mpango huo wa matibabu wenye uvumbuzi unaowapatia watu wa Afrika dawa ya Artemisinin unalingana na fikra ya undani wa matibabu ya kichina, na unaunganisha maarifa ya China na hali halisi ya mlipuko wa malaria barani Afrika. Tunawapatia watu wote dawa na kuangamiza chanzo cha ugonjwa wa malaria kwa wakati mmoja, ili kudhibiti na kuondoa ugonjwa wa malaria haraka iwezekanavyo. Matokeo ya mpango huo yametufurahisha, tumefanikiwa kudhibiti na kusimamisha mlipuko wa malaria ndani ya muda mfupi nchini humo."

    Katika mwaka 2014, Comoro imefanikiwa kutimiza lengo la kupunguza vifo vinavyotokana na malaria, idadi ya watu waliokumbwa na ugonjwa huo umepungua kwa asilimia 98% ikilinganishwa na mwaka 2006. Comoro imekuwa nchi ya kwanza ya Afrika inayofanikiwa kudhibiti ugonjwa wa malaria nchini kote ndani ya muda mfupi, ambayo wananchi wake wote walitumia dawa ya kichina kwa pamoja. Ingawa mafanikio mengi yamepatikana kutokana na "Mpango wa China katika kupambana na malaria", lakini Profesa Song Jianping bado anasisitiza kwamba kazi ya kudhibiti malaria ni kazi kubwa na ngumu kwa dunia nzima, pande zote husika zinapaswa kushirikiana na kufanya juhudi kwa pamoja ili kupata mafanikio makubwa zaidi.

    "Kwa maoni yangu, katika kazi ya kuangamiza malaria, nchi za Afrika zinatakiwa kuwa na dhamira imara, siyo tu wagonjwa wanatakiwa kuwa na dhamira, bali pia serikali inapaswa kuwa na dhamira hiyo. Kwa mfano, mafanikio ya nchi ya Comoro yanatokana na uungaji mkono wa serikali. Zaidi ya hayo, mpango wa kiutendaji pia ni jambo muhimu. Mpango wa China hasa katika kuangamiza malaria nchini Comoro kupitia kuondoa chanzo cha malaria umefanya kazi vizuri kutokana na sifa yake ya kiutendaji. Mpango huo wa kiutendaji una sifa tatu muhimu. Ya kwanza, ni kuwapatia watu dawa salama zenye ubora na urahisi wa kutumiwa; Ya pili, ni kuwashirikisha wananchi wote, kuwapatia madaktari mafunzo, kuwaelimisha wananchi ujuzi wa afya ili kuwafahamisha umuhimu wa kazi hiyo na kuwashirikisha kwa hiari; Ya tatu, ni uungaji mkono wa kutosha wa ugavi na fedha."

    Kama Profesa Song Jianping anavyosema, kundi la kupambana na malaria kutoka Chuo Kikuu cha Matibabu ya Kichina cha Guangzhou limefanya juhudi nyingi katika kuwafanya wananchi wa Comoro wafahamu na kukubali mpango wa China katika kukinga malaria, na limefanya kazi muhimu katika kutimiza lengo la kuondoa vifo vinavyotokana na malaria nchini Comoro. Mwanafunzi anayesoma shahada ya pili katika Chuo Kikuu cha Matibabu ya Kichina cha Guangzhou Wu Wanting aliwahi kushiriki kwenye kazi ya kupambana na malaria nchini Comoro mwaka 2017. Anakumbuka kazi yake akisema,

    "Naona kwamba kazi ngumu zaidi ni kazi ya matangazo wakati tulipokwenda vijijini kukusanya damu na kuwapatia dawa. Hali ya mawasiliano ya pale ni mbaya, kwa hiyo inatubidi twende vijiijni sisi wenyewe kwa kuendesha lori dogo, ili kuwafahamisha kazi yetu, na kuwapatia dawa papo hapo. Kila watakapotakiwa kula dawa tutakuja nyumbani kwao. Dawa hizo ni bure, pia tunawapatia washauri wa ujuzi wa dawa na matibabu, ili waweze kutuamini na kushirikiana nasi, hayo yote yanafanya kazi kubwa katika kutimiza lengo la kutokuwepo kwa malaria. Mpango wetu unasaidia kuangamiza Plasmodium waliomo ndani ya mwili wa watu wenye virusi vya malaria, ambao ni muhimu zaidi katika kukinga malaria kwa watu."

    Katika Mkutano wa kilele wa baraza la ushirikiano kati ya China na Afrika uliofanyika mjini Johannesburg mwaka 2015, rais Xi Jinping wa China alitoa "Mipango kumi ya ushirikiano kati ya China na Afrika" katika miaka mitatu ijayo, ikiwemo mpango wa ushirikiano kwenye sekta ya afya ya umma, "kuipatia Afrika dawa ya Artemisinin" ndiyo mambo makuu yaliyomo kwenye mpango huo, ambao unaonyesha kwamba China inatilia maanani kuiunga mkono Afrika katika kupambana na malaria. Katika miaka ya hivi karibuni, China inaendelea kuchukua hatua ya kuunganisha matumizi ya dawa ya Artemisinin na "Mpango wa China wa kupambana na malaria", na pia kupata mafanikio mengi katika nchi nyingi za Afrika licha ya Comoro.

    Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto wa Tanzania Bibi Ummy Ally Mwalimu amesema kwamba kutokana na msaada wa serikali ya China, maambukizi ya malaria nchini Tanzania yamepungua kwa kasi, anatarajia nchi hizo mbili zinaweza kuimarisha ushirikiano kwenye sekta ya afya, ili kuwanufaisha wananchi wengi zaidi.

    "Serikali ya China pia imetusaidia. Kwanza katika kufanya utafiti wa magonjwa ya malaria, kuangalia mazingira ya mbu, lakini na mwitikio wa matibabu ya dawa za malaria, kwenye eneo kubwa ambalo kupitia taasisi yetu ya uchunguzi wa magonjwa, taasisi yetu ya afya Ifakara. Tuna Taasisi ya Afya ya Ifakara kule Tanzania, imekuwa ikishirikiana na watafiti kutoka China katika eneo la kudhibiti malaria. Nafurahi kusema kwamba tumeweza kama Tanzania kupunguza maambukizi ya malaria kutoka asilimia 14 mwaka 2012 hadi asilimia 7 mwaka 2018. Kwa hivyo vita yetu dhidi ya malaria kwa kushirikiana na wadau wetu ikiwemo China inapata mafanikio makubwa. Lakini pia China imeweza kutusaidia kutupa dawa za kutibu malaria kali Artesunat, ambazo tunazipata kutoka kwao. Na hii imekuwa mchango mkubwa sana katika kuepusha vifo. Kwa hiyo matarajio yangu kuhusu ushirikiano kati ya China na Tanzania katika sekta ya afya, naona kwamba tunaendeleza hayo mambo mazuri ambayo tumekuwa tukishirikiana nayo katika zaidi ya miaka 50. Lakini kubwa tunataka sisi kujenga uwezo wetu wa kutoa huduma za matibabu ya kibingwa, hasa katika maeneo ya kipaumbele. Na pili, nataka wawekezaji wa China wakija Tanzania kuwekeza katika uzalishaji wa ndani wa dawa, na vifaa vya tiba."

    Mtaalamu wa Taasisi ya utafiti wa malaria ya Kenya Dr. Rebbeca Kiptuin amepongeza sana mafanikio makubwa yaliyotolewa na mtaalamu wa dawa wa China Bibi Tu Youyou kwenye sekta ya utengenezaji wa dawa ya Artemisinin.

    "Mnamo wa mwaka 2006, tulianza kutumia dawa ya Artemisinin. Lakini Artemisinin si dawa peke yake, imewekwa pamoja na njia ya ACT (Artemisinin Combination Therapy), yaani Artemisinin inawekwa pamoja na dawa nyingine. Sasa imesaidia sana kwa malaria, kwa sababu hatuna njia hiyo ya kuzuia kwa dawa tunayoitumia. Sasa hapa Kenya dawa hiyo ya Artemisinin bado inafanya kazi nzuri sana, ambayo inafanya kazi asilimia 95 kwa wagonjwa wa malaria. Hii inaonyesha kwamba dawa inafanya kazi nzuri sana. Tumesikia Bibi Tu Youyou amepata Tuzo ya Nobel. Tunasema asante sana kwake. Kwa sababu kama hivi sasa dawa hii haingeweza kutumika kwa watu wengi, na si Kenya peke yake, tunatumia kote Afrika, na hata huku upande wa Asia inatumika. Kazi hiyo iliyofanywa ni kazi nzuri nzuri sana, inasaidia afya ya watu."

    China inajitahidi kushiriki kwenye usimamizi wa masuala ya afya duniani, na kuupatia nguvu mpya ya uhai kwa uhusiano wa wenzi wa ushirikiano wa kimkakati wa pande zote kati ya China na Afrika. "Mpango wa China wa kupambana na malaria" unaendana na hali halisi ya Afrika, dawa ya Artemisinin imeokoa maisha ya watu wengi. Mambo hayo yote yanaonyesha busara ya China katika kuwanufaisha watu wa Afrika kwa afya zao, pia yameonyesha jukumu linalotekelezwa na China katika kushughulikia mambo ya kimataifa.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako