• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Ushirikiano kati ya China na Afrika wapongezwa na viongozi wa nchi na mashirika ya kimataifa

    (GMT+08:00) 2018-09-04 09:36:20
    Viongozi wa nchi mbalimbali za Afrika na mashirika ya kimataifa wamepongeza ushirikiano kati ya China na Afrika katika hotuba zao walizotoa jana kwenye ufunguzi wa mkutano wa kilele wa Beijing wa mwaka 2018 wa Baraza la Ushirikiano kati ya China na Afrika FOCAC, na kutarajia ushirikiano huo uzidi kuimarishwa.

    Rais Paul Kagame wa Rwanda, nchi mwenyekiti wa zamu wa Umoja wa Afrika alisema katika hotuba yake kuwa Baraza la FOCAC lililoanzishwa miaka 18 iliyopita katika msingi wa kuwa na usawa, kuheshimiana na kuahidi kujitahidi kupata maendeleo kwa pamoja, baraza hili limekuwa injini yenye nguvu kwa ushirikiano, na linatakiwa kuhusisha ajenda 2063 ya Afrika na malengo ya maendeleo endelevu.

    Amesema Afrika na China zitaimarisha ushirikiano wao katika sekta mbalimbali, ikiwemo tehama, miundombinu na biashara, pia zitashirikiana katika kulinda mazingira na kupanua mawasiliano kati ya watu na watu.

    Ametoa wito kwa nchi za Afrika kufurahia kushirikishwa kwenye miradi ya pamoja kwa kuinua uwezo wa kusimamia miradi na kuzifanya kampuni binafsi za Afrika zishiriki zaidi katika shughuli hizo.

    Rais Kagame pia amepinga tafsiri mbaya ya uhusiano kati ya China na Afrika na kusema uhusiano huo unaongezeka bila ya mtu yeyote kupata hasara , na maendeleo hayo yamewafurahisha watu wote wanaofanya biashara barani Afrika.

    Rais Hage Geingob wa Namibia, nchi mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika SADC amezitaka nchi wanachama wa SADC kushirikiana zaidi na China ili kupata maendeleo ya kiviwanda na kiteknolojia.

    Akiongea katika mkutano wa kilele wa Beijing wa FOCAC uliofanyika jana, Rais Geingob amesema FOCAC imetoa fursa nzuri kwa mazungumzo kati ya China na Afrika, ambapo pande mbili zinaweza kujadili masuala kama vile ushirikiano wa kikanda, kuwawezesha vijana na kudumisha amani na usalama. Amesema SADC inakaribisha China kuwekeza katika miradi ya sekta zinazopewa kipaumbele kama vile uzalishaji, miundombinu, usafirishaji, kilimo na utalii.

    Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika Moussa Faki Mahamat amepongeza uungaji mkono wa China kwa Afrika na kuhimiza pande hizo mbili kuunganisha zaidi mikakati yao ya maendeleo.

    Akizungumzia hotuba aliyoitoa rais Xi Jinping wa China katika mkutano wa kilele wa FOCAC wa jana, Faki amesema mipango minane ya utekelezaji na msaada wa dola za kimarekani bilioni 60 aliotangaza rais Xi ni ushahidi dhahiri wa uungaji mkono wa China kwa Afrika. Amesisitiza haja ya kuratibu juhudi kati ya Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika na pendekezo la Ukanda Mmoja, Njia Moja, na kwamba Umoja wa Afrika unaunga mkono pendekezo hilo.

    Naye katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema jana kwenye mkutano wa kilele kuwa ushirikiano kati ya China na Afrika kwenye sekta za amani na maendeleo ya kudumu na yenye haki unawanufaisha binadamu wote. Amesema kushiriki kwa Afrika kwenye Ukanda Mmoja, Njia Moja utasaidia bara hilo kutimiza malengo ya Ajenda 2063 ya Afrika.

    Wakati huohuo, mwakilishi wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa FAO Gabriel Rugalema jana huko Nairobi alisema mapendekezo yaliyotolewa na China kwenye mkutano wa kilele wa Beijing kuhusu usalama wa chakula na ukuaji wa kilimo yatasaidia nchi za Afrika kutimiza malengo yao ya kiviwanda kwa mpango uliowekwa.

    Amesema mbali na upatikanaji wa chakula, mapendekezo hayo pia yatasaidia kuifanyia mageuzi sekta ya kilimo na kuboresha maisha ya watu.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako