Mahakama kuu ya Bungoma imesitisha kwa muda utozaji wa ushuru (VAT) wa asilimia 16 kwa bidhaa zote za petroli nchini Kenya. Hii ni kufuatia kesi iliyowasilishwa katika mahakama hiyo na kundi moja la kutetea haki za kibinadamu, likilalama kwamba Waziri wa Fedha na Hazina ya Kitaifa Henry Rotich alikiuka sheria katika utekelezaji wa ushuru huo ambao umesababisha wananchi kuteta kutokana na kupanda kwa gharama ya maisha.
Kwenye uamuzi wake, Jaji wa mahakama ameagiza kesi hiyo isikilizwe tena Septemba 12, 2018, na mahakama kuu ya Kisumu.
Hazina ya Kitaifa iliagiza Mamlaka ya kudhibiti bei za mafuta ERC kuongeza bei ya bidhaa za petroli; mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa kuanzia Septemba 1, 2018, kufuatia utekelezaji wa ushuru huo.
Pendekezo hilo liko kwenye mswada wa Fedha wa 2013 uliopitishwa na bunge la kitaifa kutoza bidhaa hizo VAT ya asilimia 16.
Hata hivyo, Waziri wa Fedha Bw Henry Rotich amehakikishia Wakenya kwamba songombingo ya tozo la asilimia 16 VAT kwa bidhaa zote za mafuta ya petroli itapata ufumbuzi.Wiki jana wabunge walipitisha mswada wa Fedha 2018/2019 ili kuahirisha ushuru huo hadi 2020. Rais Uhuru Kenyatta ndiye anasubiriwa kuutia saini, Wakenya wakiwa na matumaini makuu kuwa kiongozi huyo ndiye atawanusuru kwa ongezeko la gharama ya maisha.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |