Chama cha soka Hispania, La Liga kimetuma maombi ya kuchezwa kwa mechi ya kawaida ya ligi kuu nchini humo kati ya Girona na Barcelona nchini Marekani.
Maombi hayo yaliwasiliswa kwa shirikisho la soka nchini humo na tayari yameanza kufanyiwa kazi.
Mchezo huo unatarajiwa kufanyika mwezi Januari mwakani na umeombwa uchezwe kwenye jiji la Miami.
Mipango ya kupeleka baadhi ya michezo ya La Liga nchini Marekani inaendelea baada ya La Liga kuridhia na huenda mchezo wa Girona na Barcelona ukatumika kama majaribio ya kupitishwa kwa mpango huo unaotarajiwa kuanza kwenye miaka ya karibuni.
Hata hivyo mpango huo umekuwa ukipingwa na chama cha wachezaji, baadhi ya vilabu sambamba na wachezaji wenyewe kwa kile kinachodaiwa kutoshirikishwa kwenye hatua za kuupitisha mpango huo.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |