Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya China Bw. Geng Shuang amesema, China inapinga kithabiti kitendo cha Marekani kuiuzia silaha Taiwan, ambacho pia kimekiuka sheria ya kimataifa na kanuni za kimsingi za uhusiano wa kimataifa.
Bw. Geng amesema, kitendo hicho pia kimekiuka kanuni za taarifa tatu za pamoja kati ya China na Marekani na kuharibu mamlaka, usalama na maslahi ya China.
Kauli hiyo imekuja baada ya idara ya ushirikiano wa usalama na ulinzi wa taifa ya Marekani kusema wizara ya mambo ya nje ya nchi hiyo imepitisha mpango wa kuiuzia Taiwan silaha zenye thamani ya dola milioni 330 za kimarekani. Bw. Geng amesisitiza tena kuwa Taiwan ni sehemu isiyotengeka ya China, na hakuna anayeweza kubadili nia thabiti ya kulinda mamlaka na ukamilifu wa ardhi na kupinga uingiliaji kutoka nje ya serikali ya China na watu wake. Serikali ya China inaitaka Marekani kuondoa mpango huo mara moja na kusimamisha mawasiliano ya kijeshi kati ya Marekani na Taiwan.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |