• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Waziri wa mambo ya nje wa China ajumuisha mambo ya kidiplomasia ya mwaka jana ya China

    (GMT+08:00) 2018-12-11 17:00:40

    Waziri wa mambo ya nje, ambaye pia ni mjumbe wa taifa wa China Bw. Wang Yi leo alipohutubia ufunguzi wa kongamano la mwaka huu kuhusu hali ya kimataifa na mambo ya kidiplomasia ya China, amesema kutokana na kukabiliwa na mabadiliko makubwa duniani, mambo ya kidiplomasia ya China yanasonga mbele kama meli kubwa baharini.

    Kwenye mkutano wa Baraza la Asia la Bo'ao uliofanyika mwanzoni mwa mwaka huu, rais Xi Jinping wa China alitangaza hatua mbalimbali za kufungua mlango zaidi. Maonesho ya kwanza ya kimataifa ya bidhaa zinazoingizwa China kutoka nje yaliyofanyika mwezi Novemba mjini Shanghai yalishirikisha zaidi ya kampuni 3,600 kutoka nchi na mashirika 172 duniani. Bw. Wang amesema kufungua zaidi mlango ni sauti kuu ya mambo ya kidiplomasia ya China kwa mwaka huu. Anasema,

    "Kutokana na kukabiliwa na ongezeko la vitendo vya kujilinda kibiashara, na vitendo vya upande mmoja, China inaunga mkono mchakato wa mafungamano duniani, na kulinda mfumo wa biashara huria na utaratibu wa pande nyingi. China imetoa ishara dhahiri ya kufungua mlango zaidi."

    Pendekezo la "Ukanda Mmoja, Njia Moja" limekuwa jukwaa kubwa zaidi la ushirikiano linalokaribishwa na dunia nzima. Takwimu zinaonesha kuwa thamani ya biashara kati ya China na nchi zinazohusika na pendekezo hilo imezidi dola trilioni 6 za kimarekani, na China imewekeza dola bilioni 80 za kimarekani katika nchi hizo, na umeleta ajira laki 2.4. Bw. Wang amesema, katika ushirikiano wa "Ukanda Mmoja, Njia Moja", China inafuata kanuni ya kujadili, kujenga na kunufaika kwa pamoja, kuzingatia uhifadhi wa mazingira na maendeleo yenye ubora zaidi, na kuheshimu sheria za kimataifa na nchi nyingine.

    Uhusiano kati ya China na Marekani unafuatiliwa na dunia nzima. Hivi karibuni rais Xi na rais Donald Trump wa Marekani walipokutana wakati wa mkutano wa Kundi la Nchi 20, walikubaliana kuhimiza uhusiano kati ya nchi hizo mbili uwe na uratibu, ushirikiano na utulivu zaidi, na kutoa mpango kwa ajili ya kutatua masuala yaliyopo na kuendeleza uhusiano huo. Bw. Wang anasema,

    "Miaka 40 imepita tangu China mpya na Marekani zianzishe uhusiano wa kibalozi, na tumepata mafunzo ya kutosha. Tunachopaswa kufahamu zaidi ni kuwa ushirikiano hunufaisha nchi hizo mbili, na mapambano yanadhuru pande zote. Marekani inapaswa kuona uchanya wa maendeleo ya China, na kupanua ushirikiano wa kunufaishana."

    Bw. Wang amesema hivi sasa ni wakati muhimu kwa mabadiliko ya mifumo ya kimataifa, na uchumi wa dunia uko katika njia panda. Kwa kufuata mkondo wa maendeleo ya zama, China inahimiza kujenga jumuiya yenye mustakabali wa pamoja, na uhusiano mpya wa kimataifa, ili kuanzisha mfumo wenye haki na usawa zaidi wa kuendesha mambo ya kimataifa. Mwaka 2019 utakuwa mwaka wa 70 tangu Jamhuri ya Watu wa China ianzishwe. China itasukuma mbele ushirikiano wa kirafiki kati ya nchi hizo mbalimbali kwa pande zote, kulinda utulivu na amani ya kikanda na kimataifa, kushiriki na kuongoza uendeshaji wa mambo ya kimataifa, na kuanzisha mustakabali mpya wa mambo ya kidiplomasia ya China.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako