Mkutano wa kilele wa Jumuiya ya Afrika Mashariki umepitisha ombi la Kenya la kuwa mgombea wa nafasi ya mjumbe asiye wa kudumu wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa.
Taarifa ya pamoja iliyotolewa mjini Arusha, Tanzania baada ya mkutano wa siku moja, imesema nafasi hiyo kwa Kenya itakuwa kwa miaka miwili na itaanza mwaka 2021.
Mwaka jana waziri wa mambo ya nje wa Kenya Bibi Monica Juma, alisema Kenya ilikuwa inafanya kampeni ya kuzishawishi nchi za Umoja wa Afrika kabla ya kuomba nafasi hiyo. Hata hivyo amesema ukubwa wa kampeni yake itategemea idadi ya nchi zitakazoomba nafasi hiyo, kwenye mkutano wa baraza la Umoja Mataifa utakaofanyika mwezi Septemba.
Taarifa pia inasema mkutano huo umelitaka baraza la mawaziri kuharakisha mchakato wa kuunda katiba ya shirikisho la kisiasa la jumuiya.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |