• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Kenya na Somalia zatakiwa kutafuta suluhu la kidiplomasia kuhusu mzozo wa mpaka

    (GMT+08:00) 2019-02-21 07:55:32

    Huku serikali za Somalia na Kenya zikiendelea kutafuta suluhu la mzozo wa baharini ulioibuka hivi karibuni, sasa kampuni moja ya Norway imesema ilipata sehemu hiyo inayozozaniwa kutoka Somalia na baadaye kutafuta wanunuzi wa Uingereza.

    Lakini Somalia imeendelea kusisitiza kuwa haijawahi kuuuza sehemu hiyo ya bahari kwani kesi kuhusu mmiliki halisi bado inaendelea kwenye mahakama ya usuluhishi ya kimataifa ICJ.

    Ronald Mutie anaripoti kutoka Nairobi.

    Kenya bado inasisitiza kuwa Somalia iliuza maeneo yenye mafuta kinyume cha sheria wakati wa mkutano kuhusu mafuta uliofanyika Februari 7 huko London.

    Lakini kampuni ya Spectrum Geo kutoka Norway inayojishughulisha na ushauri wa data inasema haikufanya utafiti wake kwenye maeneo yenye mzozo kati ya Kenya na Somalia.

    Makamu wa Rais wa kampuni hiyo Grahama Mayhew anasema kuwa data waliokusanya kutoka eneo la kilomiya 20,000 za mraba ilionyesha maeneo 15 yenye mafuta lakini liko tu upande wa Somalia.

    Lakini awali katibu wa kudumu kwenye wizara ya mambo ya kigeni nchini Kenya balozi Macharia Kamau wakati akimuita nyumbani balozi wa Kenya nchini Somalia alisisitiza kuwa Somalia iliuza eneo lenye mzozo kinyume cha sheria za kimataifa.

    "Kenya inamuita nyumbani balozi wake nchini Somalia jenerali mstaafu Lucas Tumbo kwa mashauriano ya dharura. Kwa kupuuza kanuni za kimataifa zilizokubaliwa kimataifa bila kujali, kuhusu kutatua mizozo ya mipaka na pia utatuzi wa mizozo ya kisiasa na kidiplomasia, serikali ya Somalia imeonyesha kuwa haijafikia ukomavu wa kisiasa na kidiplomasia kama ilivyo kwa serikali za kisasa."

    Mpaka wa Kenya na Somalia una urefu wa kilomita 682 kutoka Ras Kamboni hadi Mandera.

    Nchi hizo mbili zimekuwa zikisaidiana kupambana na kundi la Al shabaab ambalo linapinga serikali ya Somalia na kutekeleza mashambuliz nchini humo na pia nchini Kenya.

    Kenya ilipelekea wanajeshi wake nchini Somalia mwaka wa 2011 kujiunga na kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Afrika AMISOM kupambana na kundi hilo.

    Na sasa balozi Macharia Kamau anaona juhudu za pamoja za kuleta amani zinaweza kuathiriwa na mzozo huu mpya.

    "Inahuzunisha sana na inasikitisha kwamba serikali ya Somalia imechukua hatua hii dhidi ya watu na nchi ambayo imesiama na watu wa Somalia wakati wakikubwa na hali ngumu sana ya kibinadamu na kisiasa. Kenya imesimama na Somalia bila kusita hata wakati mmoja katika majukumu yake, Kenya haitakubali ardhi yake iingiliwe au iuzwe na jirani zake kwa watu wenye tama walioko kwenye nchi za kigeni."

    Wiki hii rais wa Somalia Mohamed Abdullahi Mohamed na waziri mkuu Hassan Ali Khayre walifanya mkutano na maafisa wa serikali na baadaye kuiomba serikali ya Kenya kusuluhisha mzozo huo kwa njia ya kidiplomasia.

    Pia somalia imesema hatua ya kumuita balozi wake wa Kenya nyumbani iliharakishwa na hivyo haingefanyika.

    Wito wa somalia wa kuwa na suluhu la kidiplomasia pia unaungwa mkono na baadhi ya maafisa wa Kenya.

    Bwana Adan Keynan alikuwa mwenyekiti wa kamati ya bunge kuhusu ulinzi na maswala ya kigeni.

    "Mzozo huu hautusaidii na wala hausaidii Somalia na hivyo basi ningependa kumuomba rais Uhuru Kenyatta na rais Mohamed Farmajo kuwaagiza mara moja mawaziri wao wa mambo ya kigeni kukutana na kusuluhisha swala hili ndani ya muda mfupi iwezekanavyo, ili kutatua mzozo huu."

    Somalia ilitoa malalamiko kwa mahakama ya usuluhishi ya kimataifa (ICJ) mwezi Agosti 2014, baada mazungumzo yote ya kidiplomasia kukwama.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako