• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China na Marekani zarefusha mazungumzo ya kibiashara

    (GMT+08:00) 2019-02-23 15:23:01

    Rais Donald Trump wa Marekani jana huko Washington alikutana na kiongozi wa ujumbe wa China wa mazungumzo ya kibiashara kati ya China na Marekani Bw. Liu He, akisema duru hii ya mazungumzo imepita hatua kubwa, lakini bado kuna kazi nyingi, hivyo pande hizo mbili zimeamua kurefusha mazungumzo hayo kwa siku mbili.

    Hii ni mara ya kwanza kwa nchi hizo mbili kurefusha mazungumzo tangu zianzishe mazungumzo yanayolenga kumaliza mvutano wa kibiashara kati yao, na inamaanisha kuwa zinakaribia kufikia makubaliano. Katika mazungumzo yanayofanyika mjini Washington, pande hizo mbili zimepita hatua katika uwiano wa biashara, kilimo, utoaji wa teknolojia, ulinzi wa hakimiliki za ubunifu, huduma za kifedha na mengineyo. Hata hivyo, kufikia makubaliano ya mwisho bado kunahitaji juhudi kubwa zaidi. Hivyo zimetoa uamuzi wa kuongeza siku mbili, ili kufanya majadiliano kwa kina zaidi.

    Aidha, uamuzi huo pia unaonesha kuwa, baada ya mvutano wa mwaka mmoja, China na Marekani zina nia imara ya kufikia makubaliano ndani ya muda uliopangwa. Kama rais Xi Jinping wa China alivyosema, China na Marekani haziwezi kutengana, ushirikiano unaleta manufaa ya pamoja, na mvutano unasababisha hasara kwa pande zote.

    Ofisi ya bajeti ya bunge la Marekani hivi karibuni ilisema, kama nchi hiyo ikidumisha kiwango cha ushuru wa forodha kinachotekelezwa hivi leo, ongezeko la uchumi wake litapungua kwa asilimia 0.1 kila mwaka katika miaka 10 ijayo. Wakati huohuo, serikali ya China pia imekiri kuwa mvutano kati yake na Marekani umeathiri maendeleo ya uchumi wake. Mbali na hayo, mashirika kadhaa ya kimataifa yamepunguza makadirio kuhusu ukuaji wa mwaka huu wa uchumi wa dunia. Hata baadhi ya wanauchumi maarufu wanatahadharisha kuwa uchumi wa dunia unaweza kudidimika mwaka huu au mwaka ujao.

    Katika mwezi mmoja uliopita, China na Marekani zimefanya duru tatu za mazungumzo ya kibiashara. Hali hii inamaanisha kuwa, wafanyakazi wa pande hizo mbili wanafanya juhudi kubwa zaidi, ili kutekeleza maoni ya pamoja yaliyofikiwa na viongozi wa nchi hizo mbili nchini Argentina mwishoni mwa mwaka jana wakati wa mkutano wa G20.

    Marekani na China zinashika nafasi ya kwanza na ya pili kwa uchumi duniani, na zina mvutano tatanishi wa kibiashara, ambao ni vigumu kutatuliwa ndani ya siku 90. Katika wikiendi hii, duru ya 7 ya mazungumzo kati yao itaendelea. Rais Xi wa China ametuma ujumbe kwa rais Trump wa Marekani, akisema anatumai pande hizo mbili ziendelee kujitahidi kufikia makubaliano ya kunufaishana, kwa kufuata kanuni ya kuheshimana na kushirikiana. Rais Trump alijibu kuwa anaamini pande hizo mbili zitafikia makubaliano yenye maana na ya kunufaishana, na anatarajia kufanya mazungumzo tena na rais Xi katika siku zisizo mbele sana. Kauli za marais hao zimetia nguvu kwa mazungumzo ya kibiashara kati ya nchi hizo mbili.

    Hata hivyo, kutokana na tofauti za hali ya kitaifa, mfumo wa jamii, utamaduni na desturi, China imetambua kuwa mvutano wa kibiashara kati ya nchi hizo mbili ni wa muda mrefu, na wenye ugumu na utatanishi. Bila kujali matokeo ya mwisho ya mazungumzo hayo, China itaendelea kukuza mageuzi na kufungua mlango ili kutimiza maendeleo yenye ubora zaidi ya uchumi. Kwani kufanya vizuri mambo ya ndani ni uzoefu muhimu wa China katika miaka 40 iliyopita tangu ianze kutekeleza sera ya mageuzi na kufungua mlango, na pia ni "mwavuli wake wa kuzuia mvua na upepo kutoka nje".

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako