Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (Mviwata), umewataka wajasiriamali kutengeneza bidhaa bora na zenye viwango ambazo zitauzwa bei nafuu ili kupata masoko ya uhakika ndani na nje ya nchi.
Kadhalika wametakiwa kutumia nyenzo na maarifa mbalimbali wanayopata katika mafunzo ya usindikaji wa mazao ya vyakula na mifugo.
Mratibu wa Mviwata mkoani hapa, Richard Masandika, aliyasema hayo wakati akifunga mafunzo ya usindikaji wa mazao ya vyakula na mifugo kwa washiriki 23 kutoka wilayani Karatu.
Mapema Meneja wa Shirika la Kuhudumia Viwanda Vidogo nchini, (SIDO), Mkoa wa Arusha, Nina Nchimbi, aliwasisitiza wajasiriamali wote kuwa na vitambulisho vya ujasiriamali ambavyo vinatolewa nchi nzima katika kata husika ili warasimishwe rasmi katika biashara na bidhaa zao.
Aliwataka wajasiriamali wote nchini kuhakikisha wanaanzisha viwanda vidogo vidogo na wengine kuajiriwa katika viwanda hivyo lengo likiwa ni kujiongezea kipato na uchumi wa taifa kwa ujumla ikiwamo kupunguza ukosefu wa ajira kwa vijana.
Mratibu wa mafunzo hayo kutoka SIDO, mkoani hapa, Bahati Mkopi, aliwataka wajasiriamali wote wenye nia ya kuwa na ujuzi wa kusindika mazao ya vyakula na mifugo wasisite kufika kwenye shirika hilo ili kupatiwa mafunzo na nyenzo mbalimbali.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |