• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Rais Xi Jinping wa China kuanza ziara nchini Monaco

    (GMT+08:00) 2019-03-24 18:08:26

    Kutokana na mwaliko wa mfalme Albert Alexandre Louis Pierre Grimaldi wa Monaco, rais Xi Jinping wa China leo anatarajiwa kufika Monaco na kuanza ziara rasmi nchini humo, ikiwa ni mara ya kwanza kwa rais wa China kuitembelea nchi hiyo tangu nchi hizo mbili zianzishe uhusiano wa kibalozi mwaka 1995. Ziara hiyo imetoa ishara wazi duniani kuwa haijalishi kama nchi ni kubwa au ndogo, au ziko umbali wa kiasi gani, zinaweza kuwa wenzi wa ushirikiano wa kunufaishana.

    Ikilinganishwa na China yenye eneo la kilomita za mraba zaidi ya milioni 9.6, Monaco iliyoko kando ya Bahari ya Mediterranean ina eneo la kilomita za mraba zaidi ya mbili tu, ni nchi ya pili kwa udogo wa eneo duniani. Monaco ikiwa ni nchi ya kibepari iliyoendelea, wastani wa pato la kila mtu umezidi Euro laki 1.7, na kuifanya kuwa moja ya nchi zenye kiwango cha juu zaidi cha pato la kila mtu duniani.

    Mwaka 2018, rais Xi Jinping wa China alipokutana na mfalme Albert II wa Monaco hapa Beijing, alisema ingawa China na Monaco ziko mbali, na hali zao za taifa zina tofauti kubwa, nchi hizo mbili zimejenga uhusiano mzuri kwenye msingi wa kuheshimiana, kutendeana kwa usawa na kunufaishana. Katika miaka zaidi ya ishirini iliyopita tangu China na Monaco zianzishe uhusiano wa kibalozi, uhusiano kati yao umekuwa mfano wa kuigwa wa ushirikiano kati ya nchi iliyoendelea na inayoendelea.

    Mapema mwaka 2012, shirika la mawasiliano ya simu la Monaco lilianzisha ushirikiano na kampuni ya Tehama ya China Huawei, na kujenga mtandao wa kwanza wenye kasi ya Gigabit duniani nchini Monaco mwaka 2016. Mwezi Septemba mwaka jana, pande hizo mbili zilisaini makubaliano ya ushirikiano wa 5G, na Monaco itakuwa nchi ya kwanza duniani inayounganisha maeneo yote kwa mtandao wa 5G.

    Mbali na sekta ya Tehama, China na Monaco pia zimekuwa na ushirikiano kwenye nyanja ya malipo ya kidijitali yasiyotumia pesa taslim. Mwezi Juni mwaka 2017, Monaco ilisaini makubaliano ya ushirikiano na kampuni ya huduma ya malipo ya kidijitali ya China Alipay, ili kuwarahisishia watalii wa China kufanya manunuzi na malipo nchini Monaco.

    Monaco ikiwa ni nchi yenye vivutio maarufu vya utalii duniani, Rais Xi Jinping wa China ameipongeza kwa mkakati wake wa uhifadhi wa mazingira na maendeleo yasiyochafua mazingira. Anatumai kuwa China na Monaco zinaweza kuimarisha ushirikiano kwenye nyanja za mazingira, nishati safi, mabadiliko ya hali ya hewa na uhifadhi wa wanyamapori chini ya Pendekezo la "Ukanda mmoja, Njia moja".

    Katika enzi ya utandawazi, namna ya kushughulikia mahusiano ya nje siku zote ni suala linaloikabili kila nchi na kila taifa duniani. China inapendekeza kuwa kila nchi duniani, kubwa au ndogo, tariji au maskini, zote ni wanachama sawa wa jumuiya ya kimataifa. Masuala makubwa ya kimataifa yakiwemo biashara, teknolojia, fedha, mazingira na mapambano dhidi ya ugaidi, kamwe hayawezi kutatuliwa na nchi moja peke yake, bali yanahitaji nchi mbalimbali duniani kuungana mkono, kuweka kwa pamoja utaratibu wa pande nyingi, na kukabiliana na changamoto kwa pamoja kwenye msingi wa kuheshimiana na kuaminiana.

    China ikiwa ni nchi kubwa zaidi inayoendelea duniani, inasisitiza kufuata mkakati mpya wa maendeleo yenye uvumbuzi, uratibu, kufungua mlango, kunufaishana na kutochafua mazingira. Kwa upande wa China, ingawa Monaco ni nchi ndogo kwa eneo, mkakati wake maalumu wa kuendeleza miji unaoheshimu mazingira ya asili na historia, unastahili kuigwa na China. Hali hizo zote zimetia nguvu na msukumo mpya kwa China na Monaco kuendeleza ushirikiano kati yao kwenye nyanja za "uchumi usiochafua mazingira", uhifadhi wa mazingira, huduma za fedha, maendeleo endelevu, utalii na mawasiliano ya kiutamaduni katika siku zijazo.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako