• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Watalii 343 toka China watembelea vivutio vya utalii Tanzania na kuvitangaza nchini mwao  kupitia  mkakati wa "Tour Africa New Horizon"

    (GMT+08:00) 2019-05-14 08:11:55

    VIVUTIO vya Utalii nchini Tanzania ,vitaanza kutangazwa nchini China baada watalii 343 kuwasiliTanzania kutoka China ikiwa ni matokeo ya uzinduzi wa mkakati unaojulikana kama 'Tour Africa New Horizon'.

    Hilo ni kundi la kwanza kati ya watalii 10,000 kutoka China watakaotembelea nchini mwaka huu ikiwa ni sehemu ya mkakati huo uliozinduliwa nchini China

    Watalii hao walioongozana na balozi wa Tanzania nchini China,Mbelwa Kairuki waliwasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro(KIA) na kupokelewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ,kula nao chakula cha jioni na badaye watatembelea vivutio mbalimbali vya utalii kwa siku tano.

    Mkurugenzi Mtendaji wa TTB, Devotha Mdachi anasema watalii hao ni pamoja na watu mashuhuri, wawekezaji kutoka kampuni 27 na waandishi wa habari 40 watakaotangaza sekta ya utalii kwa kutoa habari kuhusu vuivutio vya utalii Tanzania.

    Mdachi anasema miongoni mwao wapo maofisa wa serikali ya China pamoja na mawakala kutoka kampuni kubwa tatu za utalii China.

    Anasema maeneo watakayotembelea ni pamoja na Hifadhi za Taifa za Ziwa Manyara, Bonde la Ngorongoro (NCCA), Olduvai Gorge, Maasai Bomas, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na vivutio vya utalii Zanzibar kama vile Stone Town.

    "Ujio wa watalii umefanikiwa kutokana na makubaliano yaliyofikiwaNovemba, mwaka jana kati ya TTB na makampuni ya China - Touchroad International Holdings Groups wakati wa ziara ya kutangaza vivutio vya utalii Tanzania katika miji ya Beijing, Shanghai, Chengdu, Guangzhou na Hong Kong," anasema Mdachi.

    Watalii hao pia watahudhuria kongamano la uwekezaji kati ya Tanzania na China litakalofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano Arusha Centre (AICC) na kuongeza kuwa mpango wa TTB ilikuwa kutangaza vivutio vya kitalii China kupitia mikakati mbalimbali na mwezi ujao TTB itakuwa na ziara kama hiyo katika miji ya Nanjing, Hanzhou na Changsha.

    Anaishukuru serikali kwa ushirikiano mkubwa kwa bodi katika mkakati wa kutangaza sekta ya utalii nchini na kuongeza kwa namna hali inavyoendelea, TTB inatarajia kufikia malengo yake ya kuwa na watalii milioni mbili ikifikapo 2020.

    "Tunaishukuru serikali kwa ushirikiano wake, wizara ya maliasili na utalii, mamlaka za hifadhi za taifa(NCCA), Mamlaka ya Wanyapori Tanzania (Tawa), Mamlaka ya Hifadhi Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na wadau wa sekta binafsi kwa kuwezesha ziara ya watalii hao kutoka China," anasema.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako