• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Jumuiya ya kimataifa yasifu waraka uliotolewa na China kuhusu mambo ya kihistoria ya Xinjiang

    (GMT+08:00) 2019-07-23 17:11:45

    Ofisi ya habari ya baraza la serikali ya China imetoa waraka wa "masuala ya kihistoria ya mkoa wa Xinjiang", na kukosoa makundi yenye uhasama ya ndani na nje ya China kwa kupotosha historia na ukweli wa mambo ya mkoa huo. Watu wa hali mbalimbali wa jumuiya ya kimataifa wamepongeza waraka huo, wakisema mkoa wa Xinjiang ni sehemu isiyotengeka ya China, na kutokana na sera nzuri ya makabila, mkoa huo umepata ustawi na maendeleo ya mfululizo.

    Profesa Tursunali Kuzyev wa Chuo Kikuu cha Lugha za Dunia cha Uzbekistan amesema, waraka huo umedhihirisha hali halisi ya Xinjiang katika nyanja mbalimbali zikiwemo historia na dini, na kutoa majibu kwa wasiwasi na taarifa zisizo za kweli zinazotolewa na vyombo vya habari vya nchi za magharibi, ili jumuiya ya kimataifa ifahamu zaidi mkoa huo wa China. Profesa Kuzyev aliyetembelea karibu sehemu zote za Xinjiang amesema, katika miaka ya hivi karibuni, mkoa huo umedumisha maendeleo mfululizo ya uchumi na utulivu wa jamii, na wakazi wake wa makabila tofauti wanaishi maisha bora kwa masikilizano.

    Mtaalamu wa elimu za mashariki wa Russia Bw. Oleg Yakovlev amesema, China inaharakisha kutekeleza mkakati wa kuendeleza sehemu za magharibi, na kuhimiza maendeleo ya uchumi na jamii katika mkoa wa Xinjiang. Licha ya hayo, serikali ya China imehamasisha wawekezaji wa mikoa inayoendelea kuanzisha makampuni mkoani Xinjiang, ili kutoa ajira kwa wakazi wa mkoa huo.

    Mtaalamu wa mambo ya China wa Ufaransa Bi. Sonia Bressler aliyetembelea sehemu mbalimbali za mkoa wa Xinjiang amesema, waraka huo umeelezea historia na hali ya sasa ya mkoa huo, na unasaidia sana jumuiya ya kimataifa kuufahamu vizuri mkoa huo. Ameongeza kuwa baadhi ya watu wa magharibi hawafahamu mkoa huo wa China, kwa kupotoshwa na habari zisizo sahihi.

    Mtaalamu wa mambo ya China wa Saudi Arabia Bw. Abdulaziz Alshaabani amesema, juhudi za China katika kuhimiza maendeleo ya uchumi na kudumisha utulivu wa jamii mkoani Xinjiang zinastahili kuheshimiwa na kueleweka na jumuiya ya kimataifa, na pia zimezuia kuenea kwa msimamo mkali wa kidini na ugaidi.

    Profesa Nasser Abdel-Aal wa Chuo Kikuu cha Ain Shams cha Misri ambaye pia ni mtaalamu wa mambo ya China amesema, tangu enzi ya Han miaka 2,000 iliyopita, sehemu ya Xinjiang imekuwa ardhi ya China.

    Habari nyingine zinasema, wanahabari kutoka nchi 24 zikiwemo Marekani, Russia, Italia, na Japan wametembelea mkoa wa Xinjiang kuanzia tarehe 14 hadi 22 mwezi huu. Wamesema serikali ya China imepiga hatua katika kupambana na ugaidi kwa hatua zinazoendana na sheria, kulinda uhuru wa kuabudu wa wakazi, kuhifadhi utamaduni wa makabila madogo, na kuboresha maisha ya watu.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako