Kwa mujibu wa Kampuni ya uchimbaji mafuta ya Tullow Oil ,ni kuwa kiwango cha mafuta kutoka Turkana kilichofikishwa Mombasa kwa uhifadhi, sasa kimetosha kusafirishwa kwa meli hadi nchi ya kigeni kwa majaribio ya kibiashara.
Mpango huo unatarajiwa kufanikishwa kabla robo hii ya tatu ya mwaka ikamilike Septemba, ingawa haijajulikana wazi mafuta yatasafirishwa hadi nchi gani.
Kwenye ripoti ya kibiashara iliyotumwa kwa vyumba vya habari Jumatano, Tullow ilisema kufikia sasa mapipa 200,000 ya mafuta ambayo ni sawa na lita 31.8 milioni yamehifadhiwa Mombasa.
Afisa Mkuu Mtendaji wa Tullow,Bw Paul McDade,kwenye ripoti hiyo,alisema amefurahishwa zaidi na hatua zilizopigwa Kenya kwani inatarajiwa mafuta yatasafirishwa nje ya nchi hivi karibuni kwa mara ya kwanza Afrika Mashariki.
Tullow ilisema hatua kubwa zilizopigwa sasa zimeleta matumaini kwamba, Kenya itaanza rasmi biashara ya uuzaji mafuta kati ya Julai na Desemba mwaka ujao.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |