Kampuni ya teknolojia ya China Huawei imezindua programu ya kuwaongoza wanawake wanaotaka kuchukua kozi ya teknolojia ya habari na mawasiliano TEHAMA, ili kuongeza uwezo wao wa kupata ajira au kuingia kwenye ujasiriamali wa kidijitali.
Ofisa mkuu mtendaji wa Huawei nchini Kenya, Stone He, amesema programu ya kuwaongoza wanawake katika mpango wa teknolojia wa Huawei inatarajiwa kuziba pengo la jinsia katika elimu ya teknolojia nchini humo. Amesema wamegundua kuwa kuna umuhimu wa kuwapatia wanawake fursa kwenye sekta ya TEHAMA kwa kuhakikisha wanashauriwa na kupewa mafunzo ili kuwawezesha kuchukua nafasi za juu za usimamizi.
Programu hiyo ya uongozi ya Huawei ambayo ni sehemu ya jukumu la kijamii la kampuni hiyo, inalenga kukiwezesha kizazi kijacho cha wanawake wa Kenya katika teknolojia kwa kuwapatia ujuzi, vielelezo na fursa zinazohitajika kuwafanya wawe bora katika eneo ambalo linatawaliwa na wanaume.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |