Rais Xi Jinping wa China leo hapa Beijing alipokutana na chansela wa Ujerumani Bibi Angela Merkel, amesisitiza kuwa pande hizo zinapaswa kupanua ushirikiano kati yao, na kushikilia kanuni ya kuheshimiana, kufuata njia ya mazungumzo, kuheshimu njia ya kujiendeleza ya upande mwingine, na kujali maslahi makuu ya upande mwingine, ili kuwa wenzi wenye usawa wa kimkakati wa ushirikiano wa kunufaishana na mawasiliano ya kufundishana.
Rais Xi amesema hivi sasa dunia inakabiliwa na matishio makubwa ya vitendo vya kujilinda kimaslahi na vya upande mmoja, na nchi yoyote haiwezi kujitenga na hali hiyo. Amesema zikiwa nchi kubwa zinazowajibika, China na Ujerumani zinatakiwa kuongeza mawasiliano ya kimkakati, uratibu na ushirikiano kuliko zamani, ili kukabiliana na changamoto ya pamoja ya binadamu.
Bibi Merkel amesema ushirikiano kati ya Ujerumani na China unaendelea vizuri, na Ujerumani inapenda kufuata utaratibu wa pande nyingi na biashara huria, kuimarisha mawasiliano na uratibu katika mambo ya kimataifa, na kuchangia maendeleo ya uhusiano kati ya Ulaya na China.
Waziri mkuu wa China Bw. Li Keqiang siku hiyo pia amefanya mazungumzo na Bibi Merkel.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |