Baada ya Bw. Mugabe kufariki jana, rais Mnangagwa alirejea Zimbabwe kutoka Afrika Kusini alikokuwa akihudhuria mkutano wa viongozi wa Afrika wa Baraza la Uchumi Duniani. Alimsifu Mugabe kuwa mwanzilishi wa taifa la Zimbabwe, mwalimu na mwanasiasa mkubwa ambaye ni baba wa taifa aliyeiongoza Zimbabwe kupata uhuru. Ameahidi kuwa serikali ya Zimbabwe itaendelea kuhimiza mabadiliko ya jamii, kurudisha na kuendeleza uchumi ili kutimiza ustawi wa Zimbabwe mapema iwezekanavyo.
Rais wa Tanzania John Magufuli ameeleza masikitiko yake kufuatia kifo cha Bw. Mugabe akisema Afrika imepoteza mmoja wa viongozi wake shujaa, aliyepinga ukoloni kwa vitendo.
Wakati huohuo, rais Xi Jinping wa China ametoa salamu za pole kwa mwenzake wa Zimbabwe Bw. Emmerson Mnangagwa kufuatia kifo cha rais wa zamani wa Zimbabwe Bw. Robert Mugabe. Kwenye salamu zake rais Xi kwa niaba ya serikali ya China na watu wake, ametoa salamu za rambirambi kwa serikali na watu wa Zimbabwe na familia ya Bw. Mugabe.
Rais Mugabe aliyeondolewa madarakani mwaka 2017 baada ya kuwa rais kwa miaka 37, alifariki jana akiwa na umri wa miaka 95.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |