Shirikisho la Kimataifa la Msalaba Mwekundu na Hilali Nyekundu IFRC limeonya kuwa idadi ya watu wanaohitaji misaada ya kibinadamu kila mwaka kutokana na majanga yanayohusiana na hali ya hewa inaweza kuwa maradufu ifikapo mwaka 2050.
Hayo yamo kwenye ripoti iliyotolewa jana na shirikisho hilo ambayo imekadiria kuwa idadi ya watu wanaohitaji usaidizi wa kibinadamu kutokana na kimbunga, ukame na mafuriko inaweza kupanda na kuzidi milioni 200 kwa mwaka, ikilinganishwa na makadirio ya sasa ya milioni 108. Kulingana na ripoti hiyo iliyopewa jina la "Gharama za Kutochukua hatua yoyote", kuongezeka kwa idadi hiyo kutaambatana na gharama kubwa za kifedha, ambapo gharama za misaada ya kibinadamu inayohusiana na hali ya hewa itafikia dola bilioni 20 za Kimarekani kwa mwaka hadi kufikia mwaka 2030.
Akiongea kwenye mkutano wa Kilele wa Hatua za Hali ya Hewa wa Umoja wa Mataifa, rais wa IFRC Francesco Rocca amesema ripoti inaonesha gharama zilizo wazi na za kushtua za kutochukua hatua yoyote. Hata hivyo amesisitiza kuwa pia zinaonesha bado kuna nafasi ya kuchukua hatua.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |