• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Viongozi wa China waweka vikapu vya maua kwa mashujaa waliojitoa mhanga

    (GMT+08:00) 2019-09-30 17:22:15

    Leo tarehe 30 Septemba ni siku ya kuwakumbuka mashujaa wa China waliojitoa mhanga kwa ajili ya nchi na watu wa China. Hafla ya kuweka vikapu vya maua kwa mashujaa hao imefanyika kwenye Uwanja wa Tian'anmen mjini Beijing, na kuhudhuriwa na viongozi wa China pamoja na zaidi ya wajumbe 4,000 wa ngazi mbalimbali, wakiwemo askari wa zamani, maofisa wandamizi wastaafu, jamaa wa washujaa waliojitoa mhanga, watu waliopewa medali ya kitaifa, wanafunzi na watoto.

    Huu ni mwaka wa 70 tangu kuanzishwa kwa Jamhuri ya Watu wa China. Takwimu zisizokamilika zinaonesha kuwa, jumla ya watu milioni 20 walijitoa mhanga kwa ajili ya uhuru, ukombozi na ustawi wa taifa na maisha bora ya wananchi wa China. Mwaka 2014, China ilipitisha sheria na kuiweka tarehe 30, Septemba kama ni siku ya kuwakumbuka mashujaa waliojitoa mhanga.

    Saa nne kamili asubuhi ya leo, bendi ya jeshi ilipiga wimbo wa taifa, huku wajumbe wote wakiimba wimbo huo.

    Baada ya wimbo kumalizika, watu wote walisimama kimya, ili kutoa heshima kwa watu waliojitoa mhanga kwa ajili ya shughuli za ukombozi na ujenzi wa taifa la China. Kisha watoto walioshika maua waliimba wimbo wa "Sisi ni warithi wa shughuli za Ukoministi" mbele ya mnara wa kumbukumbu ya mashujaa waliojitoa mhanga. Baadaye walinzi 18 wa heshima waliweka vikapu 9 vyenye maua mbele ya mnara huo. Vikapu hivyo vilitolewa na Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China CPC, Kamati ya Kudumu ya Bunge la Umma, Baraza la Serikali, Baraza la Mashauriano ya Kisiasa, Kamati ya Kijeshi, Vyama vingine vya siasa tofauti na CPC, Shirikisho Kuu la Viwanda na Biashara pamoja na wazalendo wasio na vyama, wajumbe kutoka mashirika na hali mbalimbali, askari wa zamani, maofisa waandamizi waliostaafu, ndugu wa watu waliojitoa mhanga, na Chama cha Watoto Watangulizi.

    Rais Xi aliweka utepe mwekundu kwenye vikapu vya maua, na kuwaongoza maofisa waandamizi wengine kuzunguka mnara huo ili kutoa heshima. Watoto na watu wengine waliweka maua chini ya mnara huo.

    Kabla ya kuanza kwa hafla hiyo, viongozi wa China akiwemo rais Xi Jinping, waziri mkuu Li Keqiang, na viongozi wengine walikwenda kwenye jumba la kumbukumbu ya hayati Mao Zedong, aliyekuwa rais wa kwanza wa Jamhuri ya Watu wa China, na kutoa heshima.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako