Ethiopia, Sudan Kusini na Uganda yatanufaika pakubwa kutoka kwa mradi wa awamu ya pili wa reli mpya ya kisasa, SGR. Hii ni kutokana na kurahisishwa kwa usafirishaji wa shehena za mizigo kwa kutumia reli kutoka Mombasa hadi kwenye bandari kavu ya Naivasha. Aidha, akizindua awamu ya pili ya reli ya SGR kutoka Nairobi kuelekea Naivasha, rais Uhuru Kenyatta amesisitiza kwamba atahakikisha kuwa reli ya SGR imefika maeneo ya Kisumu na Malaba. Awamu hii ya pili ya SGR itaunganisha kaunti tano, zikiwemo Nairobi, Kajiado, Narok, Kiambu na Nakuru. Vile vile, kutakuwa na vituo vinne vya abiria ambavyo ni Ongata Rongai, Ngong, Mai Mahiu na Suswa.
Mradi huu ulioanzishwa mwaka wa 2017, umegharimu shilingi bilioni 150 na unatarajiwa kurahisisha usafiri wa maelfu ya wakenya. Kando na usafiri wa abiria, kutakuwepo na treni za kubeba mizigo, hatua ambayo itapiga jeki ustawi wa uchumi na biashara.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |