Mkimbiaji tegemeo wa mbio za marathon kutoka Kenya Patrick Cheruiyot ameripotiwa kufariki siku kadhaa baada ya kujitoa kwenye mbio za Austria. Imefahamika kuwa Cheruiyot alishiriki mbio Marathon za Graz nchini Austria wikiendi iliyopita, lakini alilazimika kujiondoa kwenye mbio hizo baada ya kukimbia kilomita 3. Cheruiyot alikuwa mwanariadha anayeibukia aliyekuwa akifanya mazoezi Kapkitony, Kenya. Katika mbio za Standard Charter Nairobi za mwaka 2018 Cheruiyot alikuwa mtu wa tano. Volare Sports, wakala wanaomsimamia Cheruiyot walisema mwanariadha huyo alilalamika kuumwa na kichwa kabla ya kulazwa hospitali ya Nairobi akiwa na Malaria. Baada ya dawa za malaria kushindwa kufanya kazi alifanyiwa CT Scan ya kichwa Oktoba 16 na kugundulika kuwa anavuja damu na ilipofika Ijumaa Oktoba 18 alifariki dunia. Mungu ailaze roho ya marehemu pema peponi, Amin.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |