Mawaziri wa afya kutoka nchi 16 wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika SADC wanatarajiwa kukutana Tanzania mwezi ujao kutathmini maendeleo yaliyopatikana katika mapambano dhidi ya magonjwa makuu yanayoathiri kanda hiyo.
Waziri wa afya wa Tanzania Bibi Ummy Mwalimu amesema mawaziri hao watapitia maendeleo yaliyopatikana katika vita dhidi ya UKIMWI, malaria, kifua kikuu, Ebola na hatua zilizochukuliwa kuelekea kuboresha hali ya lishe.
Akizungumza na wanahabari mjini Dar es Salaam kabla ya mkutano huo kufanyika kuanzia tarehe 4 hadi 8 mwezi Novemba, Bibi Mwalimu amesema kuimarisha mifumo ya afya na ugavi wa dawa kwenye kanda hiyo pia kutakuwa ni sehemu ya ajenda ya mkutano huo.
Kwa mujibu wa waziri huyo Tanzania imepata maendeleo makubwa katika kupambana na Ukimwi, na kiwango cha maambukizi ya virusi vya Ukimwi kimepungua hadi kufikia asilimia 4.7 kutoka asilimia 7 ya mwaka 2003.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |