• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Mkutano kuhusu mtandao wa nishati duniani wahimiza ushirikiano kwenye maendeleo endelevu

    (GMT+08:00) 2019-11-07 09:20:44

    Wageni zaidi ya 1,000 kutoka nchi 79 wamekutana hapa Beijing kwenye Mkutano wa Mtandao wa Nishati Duniani Mwaka 2019 na Mkutano wa Nishati na Umeme kati ya China na Afrika, wakijadili ushirikiano kuhusu maendeleo endelevu kwenye sekta ya nishati.

    Pendekezo la kujenga mtandao wa nishati duniani lilitolewa na China kwenye mkutano wa Umoja wa Mataifa kuhusu maendeleo mwezi Septemba mwaka 2015. Katika miaka minne iliyopita, pendekezo hilo limetekelezwa kwa vitendo na kuzaa matunda mengi. Hivi sasa ujenzi wa mtandao wa nishati duniani umejumuishwa na taratibu mbalimbali za kiutendaji ikiwemo kujenga "Ukanda Mmoja, Njia Moja", ajenda ya maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa mwaka 2030, kuhimiza utekelezaji wa "Makubaliano ya Paris", kuhimiza usimamizi wa mazingira duniani na kutatua matatizo ya ukosefu wa umeme, umaskini na afya. Pia kazi kuhusu mipango, teknolojia, vifaa na vigezo vya mtandao wa nishati duniani pia zimekamilika. Naibu katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Bw. Liu Zhenmin ametoa hotuba kwenye mkutano huo, akisema,

    "Mtandao wa nishati duniani unaweza kuzisaidia nchi zinazoendelea kutumia nishati safi, kuongeza kasi ya mageuzi ya sekta ya nishati, kuhimiza utimizaji wa malengo ya maendeleo endelevu, kuziwezesha nchi za Afrika kupata nishati zenye bei nafuu, safi na za uhakika, kuongeza upatikanaji wa nishati, na kutoa mchango kwa maendeleo endelevu na ujenzi wa jamii ya amani na yenye masikilizano. Mkutano huu ni fursa nzuri katika kutafuta ushirikiano, kupeana mafunzo na kutumia rasilimali za teknolojia na fedha."

    Mkutano huo pia umeangalia ushirikiano wa nishati na umeme kati ya China na Afrika na maendeleo ya mtandao wa nishati wa Afrika, kulenga kuhimiza "pendekezo la China" kutekelezwa Afrika, na kutoa nguvu mpya ya msukumo kwa utekelezaji wa "mapendekezo manne" ya ushirikiano kati ya China na Afrika. Wageni 200 kutoka nchi zaidi ya 30 za Afrika wamehudhuria mkutano huo. Naibu mkurugenzi wa idara ya nishati ya taifa ya China Bw. Liu Baohua anasema urafiki kati ya China na Afrika ni wa muda mrefu, na China na Afrika ni jumuiya yenye hatma ya pamoja na yenye maslahi ya pamoja. Mkutano huo umetoa fursa nzuri kwa ajili ya kuhimiza ushirikiano wa China na Afrika katika sekta za nishati, umeme na madini. Anasema,

    "Ningependa kutumia fursa hii kutoa mapendekezo matatu. Kwanza, kuongeza mawasiliano kuhusu sera. Kuimarisha mawasiliano, kuaminiana na ushirikiano kati ya idara mbalimbali za serikali za China na nchi za Afrika, mashirika ya kimataifa, taasisi za utafiti na makampuni mbalimbali; Pili, kuongeza mawasiliano ya kiteknolojia. Kuimarisha mawasiliano na ushirikiano kuhusu teknolojia na uvumbuzi wa mtandao wa nishati, kutumia nguvu bora ya pande mbalimbali na kufanya ushirikiano katika nadharia ya kimsingi, teknolojia muhimu na mitambo mikuu; Tatu, kuhimiza muunganiko wa miundombinu."

    Wakati wa mkutano huo, shirika la maendeleo na ushirikiano la mtandao wa nishati duniani litatoa ripoti tatu ikiwemo "utafiti kuhusu uzalishaji na usambazaji wa umeme wa maji wa Mto Kongo", "utafiti wa mtandao wa nishati wa Afrika", na "mtindo mpya wa maendeleo ya pamoja ya umeme, uchimbaji na uchakataji wa madini, viwanda na biashara", na kutoa usaidizi na ufumbuzi kwa miradi ya uendelezaji na usambazaji nje wa nishati safi na mtandao wa umeme wa Afrika.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako