Klabu za Ligi Kuu nchini Kenya (KPL) zimetakiwa zijitayarishe kwa nyakati ngumu zaidi kwa sababu hakuna matumaini ya mdhamini mpya kupatikana hadi ligi hiyo ikamilike msimu huu. Mwenyekiti wa KPL Ambrose Rachier amesema hakuna matumaini ya kupata mdhamini mpya na wale walioonyesha nia, walikuwa wakitoa pesa kidogo ambazo hazitoshi kuendesha ligi na kufadhili timu zote 18. Kwa mujibu wa Rachier ambaye pia ni mwenyekiti wa Gor Mahia, walishindwa kuafikiana na kampuni hizo zilizotoa hela chache, kwa sababu zilidai mechi za KPL hazipeperushwi katika vyombo vya habari vya kimataifa. Hata hivyo, hakufafanua iwapo KPL inafaa kusimamishwa kwa sababu taji la msimu huu bado halijanunuliwa na pia itakuwa vigumu kumtuza mshindi kwa sababu ya ukosefu wa mdhamini. Masaibu ya KPL yanatokota zaidi ikizingatiwa kwamba washindi wa taji la msimu uliopita Gor Mahia bado hawajapokezwa kitita chao hadi leo.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |