Benki ya NMB Tawi la Zanzibar imekabidhi vifaa vya michezo kwa timu za Baraza la Wawakilishi vyenye thamani zaidi ya shilingi milioni 6.5. Vifaa hivyo vitatumika katika mchezo wa mpira wa miguu, kikapu na netiboli kati ya timu ya NMB na Baraza la Wawakilishi utakaofanyika Januari 12 ikiwa ni kilele cha maadhimisho ya miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika viwanja vya Mau Zedong. Akizungumza katika hafla ya makabidhiano hayo iliyofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani, Meneja wa Benki hiyo, Abdalla Duchi, alisema lengo la utoaji wa vifaa hivyo vya michezo ni mashirikiano waliyonayo kati ya NMB na chombo hicho katika kuendeleza sekta ya michezo. Alisema Baraza la Wawakilishi mbali na kuwa na kazi ya kutunga sheria lakini pia inajishughulisha na michezo mbalimbali, ikiwemo mpira wa miguu kwa lengo la kuona Zanzibar inainuka kimichezo.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |