• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Mkutano wa Uingereza na nchi za Afrika waangalia fursa za biashara katika bara hilo baada ya Brexit

    (GMT+08:00) 2020-01-21 17:29:26

    Tarehe rasmi ya Uingereza kujitoa kwenye Umoja wa Ulaya inakaribia, na katika muda huo, serikali ya Uingereza inaangalia fursa zake za biashara ya kimataifa katika siku zijazo baada ya Brexit. Januari 20, Uingereza iliwakaribisha wajumbe wa Afrika katika mkutano wa kilele wa Uingereza na Afrika uliofanyika mjini London. Kutokana na habari zilizotolewa na Shirika la Utangazaji la Uingereza BBC, serikali ya nchi hiyo inaona fursa nzuri ya kibiashara na nchi za Afrika baada ya Brexit.

    Hii ni ishara kubwa sana kutolewa na serikali ya Waziri Mkuu wa Uingereza, Boris Johnson, anayemaanisha kuwa, hawahitaji bara la Ulaya, wanavunja vifungo vya Umoja wa Ulaya, na wanaweza kuanza kujadili makubaliano yao wenyewe na nchi nyingine. Lakini mwanahabari mwandamizi wa BBC Mathew Davies anauliza kama kweli wana fursa kama hizo za biashara kubwa na bara la Afrika. Anasema, biashara ni mtego, na makubaliano ya kibiashara ni mtego mkubwa zaidi, na majadiliano ya biashara ili kufikia makubaliano hayo ni magumu sana.

    Wakati Uingereza inajitoa kwenye Umoja wa Ulaya mwishoni mwa Januari, itakuwa bado na miezi 11 ya kufikia makubaliano ya kibiashara na Umoja wa Ulaya. Kama hawatafikia makubaliano mpaka Disemba 31, watarejea kwenye kanuni ngumu za Shirika la Biashara Duniani, WTO. Inafikiriwa kuwa Brexit itabadili mfumo mzima wa mchezo wa kufikia bei ambao utachezwa kati ya Uingereza, Umoja wa Ulaya, na nchi nyingine nje ya Umoja huo. Inadaiwa kuwa, kwa kuondoka Umoja wa Ulaya, Uingereza inaweza kufanya majadiliano ya makubaliano mapya ya biashara na pande mbalimbali, kwa sharti kuwa itawanufaisha wananchi wa Uingereza na uchumi wa nchi hiyo.

    Kuna faida nyingi za kufanya majadiliano ndani ya jumuiya moja, na kama jumuiya hiyo kufanya majadiliano na nchi nyingine. Kama BBC ilivyoweka suala hilo, kuwa sehemu ya kundi kubwa kuna faida zake na hasara zake. Unaweza kufikia maafikiano na kuweka malengo yako kuendana na sera zilizokubaliwa kwa pamoja. Lakini pia unapata nguvu ya jumuiya kuwa nyuma yako katika majadiliano ya kibiashara.

    Ingawa Uingereza itakuwa yenyewe baada ya Brexit, bado inaendelea kuwa mwanachama wa Umoja wa Forodha wa Ulaya na Soko Moja, japo mpaka Desemba 31 mwaka huu, na labda baada ya hapo.

    Hivyo, licha ya mkutano huo wa kilele wa Uingereza na Afrika unaofanyika London, biashara kati ya pande hizo mbili itaendelea kama makubaliano yaliyopo tayari kati ya Uingereza na Afrika. Baada ya mwaka 2020, mara Uingereza itakapojitoa kikamilifu kwenye Umoja wa Ulaya, makubalino ya kibiashara kati ya Uingereza na nchi nyingi za Afrika yataendelea kuwa ya kawaida chini ya makubaliano endelevu, ikimaanisha kuwa mazingira ya biashara yataendelea kuwa kama yalivyo sasa.

    Wazo moja nyuma ya makubaliano hayo endelevu, ni kwamba Uingereza itaweza kujikita zaidi kwenye majadiliano ya kibiashara na nchi ambazo hazina makubaliano hayo na Umoja wa Ulaya, kama vile Marekani. Lakini hata hivyo, bado hali ya wasiwasi inaendelea kuwepo, kwa kuwa makubaliano hayo hatimaye yatafikia mwisho, na Uingereza itahitaji kufanya majadiliano mapya na nchi mbalimbali zikiwemo za Afrika. Kwa mfano, maua ni biashara kubwa ya nje ya Kenya, ambayo kwa sasa, yanapelekwa nchini Uingereza kupitia Amsterdam. Baada ya Brexit, inawezekana kutokea tatizo la mchakato wa usafirishaji.

    Hivyo Uingereza inakabiliwa na changamoto mbili: kufanya majadiliano yenyewe, ikiwa na nguvu kidogo sana ya kufikia makubaliano, na pia vikwazo na rasilimali ya muda kwa kujaribu kujadili makubaliano ya pande mbili na nchi nyingi tofauti. Labda, kwa kugundua changamoto hizi, mkutano wa Uingereza na Afrika unaweza kutoa fursa kwa wakati kwa Uingereza kuanza mchakato mgumu na wa muda mrefu.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako