• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Wataalamu wa WHO na China wachunguza maambuizi ya virusi vya korona vya aina mpya mjini Wuhan

    (GMT+08:00) 2020-01-21 17:29:51

    Shirika la Afya Duniani WHO limesema litafanya mkutano wa dharura kesho mjini Geneva ili kutathmini kama maambukizi ya virusi vya korona vya aina mpya yanayotokea hivi karibuni nchini China ni"tukio la dharura la afya ya umma duniani" au la, na litatoa ushauri juu ya jinsi ya kudhibiti maambukizi hayo.

    Mwakilishi wa WHO nchini China Dkt. Gaduden Galea leo amesema kutokana na safari nyingi zinazofanywa na watu wakati wa sikukuu ya Mwaka Mpya wa Jadi wa Kichina itakayoanza wikiendi hii, na ongezeko la vipimo katika hospitali, huenda maambukizi ya virusi vya korona vya aina mpya yataongezeka ndani na nje ya China katika siku zijazo. Dkt. Galea amesema takwimu mpya zimeonesha wazi kuwa virusi vipya vinaweza kusababisha maambukizi kati ya watu na watu, na kesi za kuambukizwa kwa wauguzi ni ushahidi. Hata hivyo, amesema wanahitaji kufanya uchambuzi zaidi kuhusu takwimu za magonjwa ya kuambukizwa ili kujua kasi ya maambukizi.

    WHO imeushauri umma kuongeza hatua za afya ya umma na kuongeza usalama wa chakula ili kupunguza hatari ya kugusa na kuambukiza magonjwa ya aina hiyo.

    Dkt. Galea amesema hadi sasa serikali ya China imetoa maelezo kwa pande zote kuhusu virusi vya aina mpya. Baada ya kugunduliwa kwa virusi hivyo, serikali ya China imechukua hatua kuzuia maambukizi, kufunga masoko mengi yanayohusiana na maambukizi hayo, kuwaweka karantini wagonjwa, kuwafuata watu waliogusiana na wagonjwa na kufuatilia hali ya afya ya wauguzi. Vilevile, serikali ya China imefuta uwezekano wa magonjwa ya kuambukiza kama vile SARS na MERS, na kutambua virusi vya aina mpya ndani ya wiki mbili, kubadilishana habari na WHO na nchi nyingine kuhusu utaratibu wa jeni za virusi ili kuzisaidia nchi nyingine kufanya usimamizi na tiba.

    Vilevile, WHO leo imesema kwenye ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Weibo, kuwa wataalamu wa WHO wanashirikiana na wahudumu wa afya wa Wuhan kufanya uchunguzi juu ya maambukizi ya virusi vya korona vya aina mpya.

    Mjini Wuhan, timu ya uchunguzi imekutana na wataalam na maofisa wa afya wanaofanya kazi za kuchunguza maambukizi hayo. Wataalam wa WHO wamesema kuhusu aina mpya ya virusi vya korona, bado kuna mengi ya kujifunza, ikiwemo vinatokea wapi na njia za maambukizi. Sasa kazi husika zinaendelea na WHO inashirikiana kwa karibu na serikali ya China na nchi nyingine husika.

     

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako