Timu ya voliboli kwa upande wa akina dada ya Kenya Malkia Strikers itaanza kampeni yake ya michuano ya Olimpiki ya Tokyo dhidi ya wenyeji Japan Julai 26. Baada ya siku mbili Malkia Strikers, ambao wamepangwa kwenye kundi gumu 'A', watavaana na Korea kabla ya kucheza na mabingwa wa Ulaya Serbia Julai 30. Warembo hao wanaofundwa na Paul Bitok baadaye watachuana na Jamhuri ya Dominica Agosti 1 kabla ya kukamilisha hatua ya awali watakapokwaana na Brazil waliobeba medali ya dhahabu mara mbili kwenye Olimpiki Agosti 3. Kitakuwa kibarua kigumu kwa Kenya walioshindwa kuonesha cheche zao kwa wapinzani hawa katika michuano ya Kombe la Dunia mwaka jana nchini Japan ambapo walishindwa kwa seti zote. Kenya inarudi kwenye olimpiki baada ya miaka 16 kuwa nje. Wakiwashinda Botswana, Nigeria, Misri na Cameroon katika mashindano ya Afrika ya kufuzu Olimpiki yaliyofanyika Yaoundé mwezi uliopita na kujikatia tiketi iliyowekwa kwa ajili ya Afrika.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |