• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Tiba ya jadi ya kichina inapata umaarufu barani Afrika wakati wa mlipuko wa COVID-19

    (GMT+08:00) 2020-03-19 17:26:41

    Sekta ya afya nchini Namibia imetoa kibali kwa tiba ya jadi ya kichina (TCM) nchini humo. Ilimchukua Peng Wang, raia wa China anayetibu kwa kutumia dawa za asili za China mjini Windhoek, Namibia, miaka mitatu kwa tiba hiyo kusajiliwa na sekta ya afya nchini humo. Machi 6 mwaka huu, Shirikisho la Mfuko wa Msaada wa Afya nchini Namibia lilitoa kibali hicho, na kuifanya Namibia kuwa nchi ya karibuni katika mlolongo wa nchi za Afrika ambazo zinachanganya tiba ya jadi ya kichina katika mfumo wao wa afya. Uamuzi huo umekuja wakati tiba za jadi zikidhihirisha uwezo wake kuwatibu watu walioambukizwa virusi vya korona (COVID-19) nchini China.

    Nchini Namibia, madaktari katika hospitali ya Katutura iliyoko mjini Windhoek, wanashangazwa na idadi ya wagonjwa wanaovutiwa na tiba ya jadi ya Kichina. Hospitali hiyo inapokea zaidi ya wagonjwa 100 wa aina hiyo kila siku.

    Dr. Raphael Malaba, msimamizi wa Mfuko wa Bima ya Afya nchini Tanzania anasema, ni kweli kwamba hivi sasa hakuna dawa sahihi ya kutibu virusi vya korona. Hata hivyo, amesema kwa kuwa dunia inatafuta chanjo bora ya kinga na njia za matibabu, tiba ya jadi ya China imechukua nafasi kubwa nchini China katika mapambano dhidi ya virusi hivyo, na anaamini kuwa hatua hiyo inaweza kuchukuliwa kama mfano kwa nchi za Afrika katika kudhibiti mlipuko wa virusi vya korona. Dr. Malaba amesema, imeonyeshwa katika tafiti mbalimbali nchini China kuwa kwa wagonjwa walio katika hatua za mwanzo za maambukizi, matumizi ya tiba ya jadi ya Kichina pekee ilitosha kupunguza homa, dalili na athari za virusi, huku kwa wale wagonjwa wenye hali mbaya, matumizi ya tiba hiyo kwa pamoja na dawa nyingine za kutiba virusi ziliweza kuwasaidia wagonjwa hao kupona. Ameeleza matumaini yake kuwa nchi nyingi zaidi, hususan kutoka barani Afrika, zitatumia uzoefu huo na kufanya utafiti zaidi ili kuwasaidia wananchi wao.

    Kituo cha Kudhibiti na Kukinga Magonjwa cha Afrika (AfricaCDC) kimesema, bara hilo linakabiliwa na hali ngumu kwa kuwa mpaka kufikia jana, zaidi ya kesi 500 za maambukizi ya virusi vya korona zimethibitishwa katika nchi 31 kati ya 55 ambazo ni wanachama wa Umoja wa Afrika. Nchi nyingi zimeomba msaada kutoka China na kuonyesha utayari wa kujifunza kutokana na uzoefu wa nchi hiyo. Kwa miongo kadhaa, timu za madaktari wa China barani Afrika ziliweka sifa isiyopingika katika matumizi ya tiba ya jadi ya Kichina kutibu magonjwa, mengi kati yao yakiwa ni sugu na magumu.

    Dr. Mohammed Ibrahim, aliyepata mafunzo nchini Marekani anayefanya kazi kjatika hospitali ya Eastern and Western mjini Abuja, Nigeria, ameliambia Shirika la Habari la China Xinhua kuwa, tiba ya jadi ya Kichina imekubalika na kupokelewa vizuri na watu nchini Nigeria, na kuongeza kuwa idadi kubwa ya taasisi za afya zinatoa tiba hiyo. Amesema nchi nyingi zinazopambana na maambukizi ya COVID-19, ikiwemo Nigeria, zinachukua ujuzi kutoka utaratibu makini wa China. Amesema China iko wazi kuhusu ukweli na hatua, na nchi hiyo inatarajiwa kutoa maelezo zaidi kuhusu athari halisi za tiba ya asili ya Kichina kwa ugonjwa huo.

    Ikiwa bado inapambana na maambukizi ya virusi vya korona nyumbani, China inaunga mkono na kusaidia nchi za Afrika na mashirika ya kikanda kadri inavyoweza, na kupongezwa sana na nchi hizo. Jumatano mchana, wataalam wa China na maofisa kutoka idara za afya na forodha walibadilishana taarifa na uzoefu kuhusu virusi hivyo katika mkutano uliofanyika kwa njia ya video na maofisa na wataalam wa afya kutoka Africa CDC na nchi 24 za bara hilo, ikiwa ni kuonyesha nia yake ya kutoa uzoefu wake na kuiunga mkono Afrika katika mapambano dhidi ya mlipuko wa virusi vya korona. Kampuni za China na mashirika ya kiraia pia yametoa misaada ya dharura inayohitajika kwa nchi za Afrika. Jumatatu wiki hii, Jack Ma, mwanzilishi mwenza wa Kundi la Alibaba la China, alisema kuwa mfuko wake utatoa vifaa mbalimbali ikiwemo maboksi milioni 1.1 ya vipimo na mavazi ya kujikinga kwa nchi 54 za Afrika kuzisaidia kupambana na maambukizi ya virusi vya korona.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako