Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA) limepitisha azimio kuhusu virusi vya Corona (COVID-19), na kutoa wito wa kufanya ushirikiano wa kina wa kimataifa katika kupambana na janga la virusi hivyo.
Azimio namba 74/270 linaelekeza kuwa, nchi 193 wanachama wa Baraza hilo wameeleza wasiwasi wao wa tishio kwa afya ya binadamu, usalama na ustawi linalosababishwa na virusi vya Corona, ambavyo vinaendelea kuenea duniani.
Baraza hilo limetambua athari zisizotarajiwa za janga hilo, ikiwemo kuvurugika kwa jamii na uchumi, na pia usafiri duniani na biashara, na athari mbaya kwa maisha ya watu. Pia Baraza hilo limetambua kuwa janga hilo linahitaji majibu ya pamoja ya jamii ya kimataifa katika msingi wa umoja, mshikamano na ushirikiano mpya wa pande nyingi.
Kutokana na hali hiyo, Baraza hilo limetaka ushirikiano wa kina katika kudhibiti, kukinga na kushinda janga hilo, ikiwemo kwa kupitia kubadilishana taarifa, ufahamu wa kisayansi, na njia bora zaidi na kwa kutumia miongozo sahihi inayopendekezwa na Shirika la Afya Duniani.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |