• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Kiwango cha kupona kwa wagonjwa wa COVID-19 chafikia asilimia 94 nchini China

    (GMT+08:00) 2020-04-22 19:10:35

    Ofisi ya Kamati ya Afya ya Taifa ya China leo imefanya mkutano na waandishi wa habari uliohusu kukabiliana na virusi vya Corona, na kusema mbali na hali ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya Corona kuboreka ndani ya nchi, China itaimarisha kazi ya kuzuia virusi kuingia nchini katika miji inayopakana na nchi za nje.

    Ofisa wa Kamati hiyo Guo Yanhong amesema, matibabu ya wagonjwa wa virusi vya Corona za China yamepata mafanikio makubwa. Anasema,

    "Hadi sasa wagonjwa wa virusi vya Corona zaidi ya elfu 77 wamepona na kutoka hospitali, na kiwango cha kupona kwa wagonjwa wa virusi hivyo nchini China kimefikia zaidi ya asilimia 94."

    Kwa mujibu wa mpango kazi uliotolewa na serikali ya China, baada ya kutoka hospitali, wagonjwa wa virusi vya Corona wanatakiwa kuendelea kuwekwa karantini kwa siku 14 ama kwa kujitenga majumbani au kupelekwa katika eneo maalum. Hospitali zilizotengwa kukabiliana na ugonjwa huo zinawapangia wagonjwa hao ratiba ya wiki mbili ama wiki nne ya kukutana na daktari na kufanyiwa vipimo tena. Kwa wale wanaoonesha dalili za homa au kukohoa, ama kuthibitishwa bado wana virusi mwilini mwao, watarudishwa tena hospitali kwa ajili ya matibabu zaidi.

    Mkurugenzi wa kitengo cha magonjwa ya kuambukiza katika Hospitali ya Beijing Nambari 1 Wang Guiqiang amesema, wengi wa wagonjwa waliokutwa na virusi tena baada ya kupona na kutoka hospitali hawana dalili, lakini bado wanaweza kuwaambukiza watu wengine, hivyo wanatakiwa kuendelea kuchunguzwa katika eneo la kujitenga.

    China ina mpaka wa nchi kavu wenye umbali wa kilomita elfu 22.8 na inapakana na nchi nyingi. Kutokana na hali ya maambukizi ya virusi vya Corona kuzidi kuwa mbaya katika nchi za nje, baadhi ya sehemu nchini China zinakabiliwa na shinikizo kubwa la kuzuia virusi kuingia kutoka nje.

    Kamati ya Afya ya Taifa ya China imeitaka mikoa 9 yenye forodha za nchi kavu kujiandaa vizuri, na kwamba kila forodha inatakiwa kuwa na mpango wake wa kipekee, kuinua uwezo wa kuzuia virusi kuingia kutoka nje, uwezo wa kutoa matibabu na uwezo wa kudhibiti kuenea kwa virusi. Vilevile Kamati hiyo imepeleka wataalam kwenda katika sehemu hizo. Ofisa wa Kamati ya Afya ya Taifa ya China Guo Yanhong anasema,

    "Kwa mfano katika mji wa Suifenhe, tumepeleka vikosi vya madaktari pamoja na wataalam wa kudhibiti maambukizi ya virusi na maabara ili kusaidia mji huo kufanya kazi husika. Pia tumepeleka mashine kama CT ya kuhama ili kudhibiti virusi kuingia kutoka nje."

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako