Timu ya Gor Mahia almaarufu K'Ogalo ya nchini Kenya imeanza mikakati ya kujitayarisha kwa msimu ujao huku kocha Steven Polack akitarajiwa kukisuka upya kikosi chake ili kuiwezesha timu hiyo kutamba kwenye mashindano ya Bara Afrika. Polack alisema kwamba ana habari huenda wachezaji wake tegemeo wataondoka kutafuta ujira kwingine, ndiyo maana ameanza kujipanga mapema kwa ajili ya msimu ujao. Gor ambayo imekuwa ikabiliwa na matatizo chungu nzima ya kifedha, huenda ikawapoteza wachezaji wake mahiri msimu ujao iwapo hawatapata mdhamini mpya. Kipa wa timu hiyo David Mapigano, na winga Dickson Ambudo wote kutoka Tanzania na Juma Balinya kutoka Uganda tayari wametishia kwamba watakatiza huduma zao na K'Ogalo iwapo hawatalipwa malimbikizo ya mishahara yao. Pia kumekuwa na madai kwamba wachezaji kutoka Kenya ambao hawajaridhishwa na ukata ndani ya K'Ogalo wapo mguu moja nje ya mabingwa hao mara 18 wa KPL.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |