Huku mashirika ya ndege na safari za kimataifa zikitarajiwa kuanza nchini Kenya wikendi hii, serikali imebaini kuwa huenda wageni kutoka nje wasiende karantini.
Waziri wa utalii nchini humo Najib Balala ametangaza kwamba, huenda serikali ikalegeza kamba kuhusiana na hitaji la wageni watakaotoka nchi za nje kuwekwa kwenye karantini ya lazima ya siku 14.
Hayo yanajiri huku kampuni kadhaa za ndege za kimataifa zikitangaza mipango ya kuanzisha tena safari zao nchini humo.
Hatua ya serikali kutoweka wageni karantini imenuia kufufua sekta ya utalii ambayo imeathirika pakubwa kufuatia janga na virusi vya corona.
Hoteli nyingi za utalii bado zimefungwa huku wafanyikazi wakiachwa bila ajira na mapato.
Mashirika manne ya ndege za kimataifa ikiwemo KLM, British Airways, Air France na Qatar Airways zimetangaza kwamba wako tayari kuanza safari zao nje na ndani ya Kenya mnamo Agosti 1.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |