Hivi sasa kuna viwanda 170 ambavyo vimeanzishwa chini ya EZPA nchini humo na zaidi ya asilimia 40 ya viwanda hivyo vimejikita katika kuchakata na kuongeza thamani ya mazao.
Meneja wa Uhamasishaji, Uwekezaji wa EPZA, Grace Lemunge, amesema kuongeza uwekezaji katika viwanda vya uchakataji mazao kunaongeza thamani ya mazao na kumhakikishia mkulima soko la uhakika na ongezeko la kipato.
Alisema mwekezaji katika maeneo maalum ya uwekezaji ya EPZ na SEZ, anafaidika na motisha maalum inayotolewa na mamlaka pamoja na kurudisha upesi mtaji aliowekeza.
Ameongeza kuwa sekta ya kilimo inaajiri zaidi ya asilimia 70 ya watu na huchangia asilimia 30 ya Pato la Taifa, hivyo uwekezaji katika viwanda vya kuchakata mazao unamhakikisha mkulima soko la uhakika na kuongeza uzalishaji. Tanzania bado ina ardhi kubwa ambayo inafaa kwa kilimo na ambayo haijalimwa hivyo uwepo wa viwanda vya kutosha vya uchakataji ni kichocheo muhimu cha kuwafanya wakulima waongeze uzalishaji wa mazao ya kilimo.
Mamlaka ya EPZA inafanya kazi kwa karibu sana na viwanda vya kuchakata mazao kama vile dengu, mbaazi na choroko yenye soko kubwa India na nchi nyingine za Asia. Mamlaka hiyo huwaunganisha wakulima na viwanda hivyo na kupata soko la uhakika.
Awali, mazao haya yalikuwa yanatumika kwa ajili ya chakula pekee, lakini sasa ni chanzo kikubwa cha mapato kwa wakulima.
Hivi karibuni serikali ya Tanzania ilianza ujenzi wa kituo kikubwa cha biashara cha Kurasini ili kuibadilisha na kuifanya sekta ya kilimo kuwa ya kibiashara.
Mradi wa ujenzi wa kituo hicho ambacho kinatarajiwa kuwa kikubwa nchini na katika eneo lote la a Afrika Mashariki, unatekelezwa na EPZA kwa thamani ya zaidi ya Sh. bilioni 60.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |