Wafanyabiashara mjini Dodoma wametakiwa kuheshimu makubaliano ya awali ya kutopanga bidhaa zao barabarani kwa ajili ya soko. Ofisa masoko wa jiji la Dodoma James Yuna aliyasema hayo jana alipokuwa akizungumza na wafanyabiashara hao kwenye mkutano mkuu wao na kuwataka kuheshimu na kutii maelekezo yaliyoelekezwa kwao kwa ajili ya matumizi ya barabara hiyo ya Nyerere Square.
Alisema baadhi ya wafanyabiashara wanakiuka maelekezo ambayo yametolewa na halmashauri ya jiji, yanayowataka biashara zianzie kuuzwa muda wa jioni badala majira ya asubuhi.
Kwa mujibu wa Yune, barabara hiyo kwa muda wa asubuhi imetengwa ili itumike kupaki magari ambayo huliingizia jiji mapato. Yune ameongeza kuwa serikali kwa kushirikiana na halmashauri ya jiji, inawathamini wamachinga wote, hivyo kinachotakiwa ni kutii mamlaka husika ili wafanye biashara zao kwa uhuru bila kubughudhiwa.
Hata hivyo wafanyabiashara hao wameiomba halmashauri ya jiji kuruhusu siku za Jumamosi na Jumapili wafanye biashara zao kuanzia majira ya asubuhi ili kujiongezea kipato zaidi.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |