Kiwango cha maziwa nchini Kenya kimeshuka kwa asilimia 36 tangu mwezi Januari.
Waziri wa Kilimo,Peter Munya amesema upungufu huo umesababishwa na janga la Covid-19 ambalo limelisukasuka soko.
Alizungumza hayo jana jijini Nairobi wakati akitoa taarifa kuhusu athari za janga la Corona katika sekta ya maziwa nchini Kenya.
Alisema janga la Covid-19 liliharibu soko la maziwa kufuatia kufungwa kwa shule na mahoteli na hatimaye wakulima wakazembea katika uzalishaji.
Aidha alisema serikali huenda ikalazimika kuagiza maziwa ili kukidhi mahitaji kwa sababu wasindikaji maziwa sasa hivi hawana maziwa ya kutosha yanayoweza kutosheleza mahitaji ya soko.
Alisema mwezi Januari,uzalishaji ulikuwa lita milioni 63 kwa mwezi,lakini sasa uzalishaji umeshuka hadi lita milioni 42 kwa mwezi.
Aliongeza kuwa mahitaji ya kitaifa ya maziwa kwa mwezi ni lita milioni 54,kwa hivyo kuna upungufu wa lita milioni 12.
Kenya ina mojawapo ya sekta kubwa ya maziwa barani Afrika,inayozalisha lita bilioni 5.2 kwa mwaka na yote hutumika nchini.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |