• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • HATIMAYE NIMEUONA UKUTA MKUU WA CHINA…

    (GMT+08:00) 2016-08-25 15:51:20

    Na Elias Mhegera, Beijing

    Kabla ya kufika kwenye 'Ukuta Mkuu wa China' niliwahi kusoma habari za mitandaoni na kutazama video zikisema, kuijua dunia kunaendana na mambo yafuatayo:

    Kwanza ni kuwa na elimu inayoendana na dunia ya sasa, pili ni kuitembelea dunia yenyewe yaani usiwe mtu wa kuishia kwenye ramani ya nchi yako pekee, bali pia kuyatembelea maajabu ya dunia, na kuwa na uelewa wa lugha za kimataifa walau moja au mbili, mbali na lugha yako.

    Licha ya kuwa naunga mkono dhana hiyo, nakiri kwamba sidhani naweza kufanikiwa kuyakamilisha yote, lakini walau moja nimelitimiza, yaani kuyatembelea miongoni mwa maajabu ya dunia. Na kwa maana hiyo miongoni mwa kumbukumbu zangu za utalii ambazo naamini ni watu wachache nchini kwangu Tanzania watazipata, ni hili la kutembelea "Ukuta Mkuu wa China".

    Kwa bahati mbaya sisi tulitembelea ukuta huo siku yenye mvua na ukungu kwa hiyo picha zimekuwa nyeusi, lakini nimechota baadhi ya picha mitandaoni ili kuwaonesha hali halisi ya ukuta huo.

    Ukuta huu ambao ni moja ya maajabu ya dunia ya kazi mikono ya mwanadamu, ulijengwa zaidi ya miaka 221 kabla ya kuzaliwa kristu kwa lengo la kujilinda dhidi ya mashambulizi ya makabila watu kutoka kaskazini mwa China.

    Ukuta huo umeanzia mashariki na kuelekea magharibi ukipita kwenye milima na mabonde。Ni askari wachache tu walikuwa wanakaa kwenye maeneo maalum ya mlima huo, na ili kutoa tahadhari pindi wavamizi wanapokuja. Walinzi waliokaa kwenye vidungu vilivyoko kwenye ukuta huo, wakiona maadui wliawasha moto na kufukisha moshi, ili kutoa tahadhari kwa askari, ambao walifika haraka kuzia mashambulizi. Hili ni jambo unaloweza kujifunza na kuelewa ukiuona ukuta huo.

    Kutokana na kuwepo kwa muda mrefu na kuharibiwa na matukio ya asili kama vile mvua, upepo na matetemeko, baadhi ya maeneo ya ukuta huo yamejengwa upya au kukarabatiwa na tawala za enzi mbalimbali za China, hasa kati ya miaka ya 1368-1644. Kuna baadhi ya picha mbalimbali zinazoonesha ukarabati wa ukuta huo mara baada ya kuanguka kutokana na uchakavu.

    Nina haki ya kujipongeza kabla hata sijapongezwa na mtu mwingine, kwa sababu katika kundi letu la wanahabari 22 tuliokwisha vuka miaka 50 tupo watatu, lakini ni mimi peke yangu kati yao niliyeweza kufikia "Ngome ya 12".

    Ukuta huo ulikuwa mrefu sana umbali wa kilomita 21,196.18 (sawa na maili 13,170.7) na kama ungetaka kutembea toka ulipoanzia hadi mwisho wake basi ingekuchukuchua siku sita ukitembea bila kupumzika. Kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya utalii, serikali ya sasa ya China imekarabati eneo lililotumika kwa ajili ya kupanda na kuvikarabai vidungu vya kupumzikia.

    Vidungu hivyo vinaitwa fortresses kwa lugha ya Kiingereza Ngome na kwa jumla vipo 12 kwa hiyo kiutalii ukifikia cha 12 unakuwa umefikia kileleni (wakati wa kupanda), kwani baada ya hapo njia inakuwa tambarare .

    Kivutio hiki pekee cha utalii hutembelewa na watalii zaidi ya milioni 10 kwa mwaka. Pamoja na kuchoka sana na vile vile kuishiwa pumzi wakati wa kupanda, nilijikongoja na mara nilipofikia kituo cha 10 au fortresses kama vinavyofahamika nikasikia kelele kubwa A HERO na mzungu mmoja akaja kunishika mkono nikiwa nimebakiza ngazi tano hivi.

    Ni tabia ya wapanda milima kumshika mkono mtu anayemalizia ikiwa ni alama ya kumpongeza na pia kumuita A HERO yaani shujaa. Walau kwa sasa nina medali ya kuupanda ukuta huo wa kihistoria!

    Ujumbe: "Si wenye kasi kubwa au wenye nguvu pekee wawezao kuvifikia vilele, bali wenye ustahimilivu mkubwa hatua kwa hatua katika maisha…!

    Nikiwa katika sehemu mbali mbali za ukuta huo

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako