• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Sasa mitandao ya intaneti yabadilisha maisha ya watu

    (GMT+08:00) 2016-09-02 15:30:01

    Na Elias Mhegera, Beijing

    Katika ziara zangu sehemu mbali mbali za Jamhuri ya watu wa China nimevutiwa na mambo mengi, lakini suala la usalama limekuwa na umuhimu wa kipekee.

    Mfano halisi ni pale tulipolitembelea jimbo la Ningxia na tukapata mafunzo ya hali ya juu jinsi ambavyo mtandao wa intaneti unaweza kutumika ili kuyabadilisha maisha ya mwanadamu.

    Ni mahali hapo ambao unaweza kuona kwamba suala la kuwa katika mtandao wa intaneti muda wote si starehe, bali ni la msingi kama ilivyokuwa kula au kupumua.

    Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Habari katika jimbo hilo Bw. Xu He, kila mgeni ni lazima ajitambulishe kwenye mamlaka husika katika kipindi kisichozidi saa moja toka anapoingia hapo jimboni.

    Kwa maana nyingine wakazi wote wa jiji la Yinchan wamerekodiwa katika mtandao, wageni wanaofikia majumbani hurekodiwa kwa viongozi wa mitaa na kwa wale wanaofikia katika mahoteli basi ni jukumu la wenye hoteli kutoa ripoti kwa vyombo husika huku namba za pasipoti zao zikirekodiwa pia.

    "Ni kwa mtindo huo iwapo atakuja mtu mwenye rekodi ya uhalifu popote ndani ya Jamhuri ya Watu wa China taarifa zake zitamfuata mara baada ya jina lake kuingizwa mtandoni." Anasema kiongozi huyo.

    Bw. Xu ambaye pia hushughulika na udhibiti wa taarifa zote kwa njia za maandishi kama vile barua za kiofisi na masuala mengineyo ya mtandao, anasema mfumo huo umesaidia sana katika kuzuia uhalifu jimboni kwake na hasa katika makao makuu ya jimbo.

    Lakini mfumo huo wa taarifa siyo kwa wanadamu peke yao bali hata kama mkazi amefuga mbwa na paka ni lazima wasajaliwe na kila wanapodungwa sindano za kuzuia maradhi ni lazima taarifa ziingizwe mtandaoni.

    Uzuri wa mfumo huo ni pale mtu anapojaribu kudanganya kwani kompyuta itatoa taarifa ikifahamisha kwamba kuna muingiliano wa taarifa na hata kutoa picha ya mhusika wa mkanganyiko huo.

    Na iwapo kutakuwapo na mtu mwenye madeni ya umeme au maji basi mfumo huo utatoa taarifa zake. Kinachofanyika ni mhusika wa bili hizo kubonyeza kitufe cha mtaa kisha taarifa zote husika hujitokeza.

    Mfumo huo umesaidia kwa mambo mengi kama vile kuzuia uhalifu, kuzuia ajali za barabarani kwa sababu kuna kamera maalumu, kutoa taarifa za nyumba zilizopo wazi kwa ajili ya wapangaji, na vivutio vyote vya utalli katika eneo hilo.

    Habari njema pia ni kwamba biashara za mtandao ni za uhakika kwa sababu mtu anaweza kuagiza chochote akitakacho na katika muda usiozidi saa moja anaweza kuwa ameletewa tayari mahitaji yake.

    Lakini licha ya ununuzi na utalii hata watafiti wakifika katika eneo hilo huwa na kazi rahisi kwa sababu taarifa zote zimo ndani ya mtandao. Kwa kiwango kikubwa matumizi ya karatasi katika kuandika yamepungua sana kwa sababu ya kuwekwa kila taarifa mtandaoni na kwa maana hiyo pia miti imeokolewa.

    Mtandao huo umesaidia hata katika huduma za usafirishaji hususani kupeleka taarifa za mzigo unaosafirishwa, lakini pia daktari anaweza kutoa huduma ya ushauri kwa kutumia mtandao huo huo.

    Katika ujumla wake matumizi ya mtandao yamebadilisha kabisa maisha ya wakazi wa jiji la Yinchan

     

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako